2013-05-28 07:39:59

Changamoto ya maisha na utume wa Kanisa nchini Madagascar


Wananchi wa Madagascar wanaendelea kuishi katika umaskini wa kipato licha ya kuwa na utajiri mkubwa wa maliasili, madini na nishati ambayo ingetumika kwa ajili ya mafao na maendeleo ya wengi. RealAudioMP3

Hali hii inakuzwa pia na migogoro, kinzani na machafuko ya kisiasa ambayo yamekuwa yakijirudia rudia nchini humo kwa miaka kadhaa kiasi kwamba, wananchi wameanza kukosa imani na wanasiasa ambao kimsingi wamekuwa wakijali zaidi masilahi binafsi kuliko hata ustawi na maendeleo ya wananchi wa Madagscar.

Uchaguzi mkuu ambao umekuwa ukifikiriwa na wengi kuwa ni mkombozi wa hali ya kisiasa nchini Madagascar umekuwa ukihairishwa mara kwa mara kutokana na ukata na hali ngumu ya uchumi. Lakini jambo la kushangaza ni kuona kwamba, Makampuni ya Kimataifa yanaendelea kuwekeza na kupata faida kubwa katika vitega uchumi vyao, wakati ambapo wananchi wa Madagascar wanaendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini wa hali na kipato.

Kuna huduma duni za afya na elimu zinazotolewa na Serikali na kwamba, haki msingi za binadamu ziko mashakani. Hali ya maisha ni mbaya zaidi vijijini ambako kuna idadi kubwa ya watoto wanaopoteza maisha kwa magonjwa ambayo yangeweza kupatiwa kinga na tiba.

Katika mazingira kama haya anasema Askofu Rosario Vella kutoka Madascar wakati wa mahojiano maalum na Shirika la Kipapa la Misaada kwa Kanisa hitaji kwamba, Kanisa nchini humo limejikuta likibeba dhamana kubwa katika utoaji wa huduma ya elimu, afya na maendeleo endelevu, kwa kutumia kwa ukamilifu rasilimali iliyopo.

Wananchi wengi wa Madagascar kama hata ilivyo sehemu nyingine za Bara la Afrika, wanaendelea kuathirika na utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia kiasi kwamba, wanajikuta wakipoteza tunu msingi za maisha ya kifamilia, kijamii na kiutu; Upendo, mshikamano pamoja na thamani yautu wa mwanadamu si kati ya mambo yanayopewa msukumo wa pekee nchini humo. Watu wanajikuta wakielemewa na ubinafsi, uchu wa mali na madaraka hata kwa njia za mkato na kwamba, wazazi na walezi wanaanza kukosa dira na mwelekeo katika makuzi na elimu kwa watoto wao!

Kanisa Katoliki nchini Madagascar linaziona changamoto hizi na linazifanyia kazi katika maisha na utume wake, kwa kuwekeza katika majiundo ya vijana kwa njia ya elimu makini, kwani kutokana na umaskini wa kipato, vijana wakiwa bado na umri mdogo wanajikuta wakilazimika kuzikimbia familia zao hasa kwa wale wanaoishi vijijini ili kwenda mijini kutafuta nafuu na uhakika wa maisha, jambo ambalo linawanyima haki ya kuendelea na masomo pamoja na uwezekano wa kupata malezi bora kutoka katika familia husika.
Vijana hawa wanajikuta wakiishi katika mazingira magumu hali inayowapelekea kujiingiza katika matumizi haramu ya dawa za kulevya, biashara ya ngono, wizi na ujambazi. Wakati mwingine, wazazi wasiokuwa na soni wamejikuta wakiwatumbukiza watoto wao hata katika utalii wa ngono nchini Madagascar, jambo ambalo linadhalilisha utu na heshima ya wasichana na wavulana hao.








All the contents on this site are copyrighted ©.