2013-05-27 12:11:35

Uongozi hi huduma ya upendo na mshikamano!


Wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume wamehitimisha mkutano wao wa themanini na moja, uliopembua pamoja na mambo mengine, umuhimu wa huduma ya uongozi katika hija ya maisha ya kitawa kwa nyakati hizi. Ni tafakari iliyokuwa inaangalia dhamana ya uongozi mintarafu maisha ya kitawa, miaka hamsini ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Wajumbe wameshirikishana: mawazo, mang'amuzi na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha na utume wao.

Wajumbe kwa namna ya pekee wamekumbushana kwamba, mmomonyoko wa maadili na utu wema bila kusahau athari za myumbo wa uchumi kimataifa ni mambo yanayoukumba ulimwengu, Jamii na hata Kanisa, bila kusahau Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, changamoto kwa watawa kujikita zaidi na zaidi katika: mang'amuzi, uwajibikaji wa pamoja na uaminifu.

Mkutano huu umehudhuriwa pia na viongozi wakuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Wajumbe wamekumbushwa kwamba, uongozi katika maisha ya kitawa na kazi za kitume ni muhimu sana unaohitaji fadhila ya unyenyekevu na mabadiliko ya mawazo. Aishangazi kuona kwamba, kuna mgogoro wa uongozi katika Mashirika ya Kitawa kuanzia kwenye Jumuiya, hali ambayo inatishia umoja, upendo, mshikamano na uaminifu wa karama miongoni mwa watawa.

Kuna haja kwa wakuu wa mashirika ya kitawa na kazi za kitume kutambua kwamba, kuna tatizo la uongozi, linalohitaji watawa kuliangalia kwa mtazamo mpya, licha ya kukazia utii, uwajibikaji pamoja na utii wa kiimani ambao ni muhimu sana katika mchakato wa maisha miongoni mwa watawa. Viongozi wamehamasishwa kujenga na kukuza uhusiano fungamanishi miongoni mwao, ili kwa pamoja waweze kufanya hija ya maisha ya kitawa inayofumbata utu na ubinadamu unaopaswa kuinjilishwa.

Jumuiya iwe ni mahali pa majadiliano ya kina na uwajibikaji; pawe ni mahali ambapo upendo na huruma ya Mungu unamwilishwa miongoni mwa wanajumuiya. Watawa watambue kwamba, wao ni zawadi kwa jirani zao wanaotembea kwa pamoja katika kutekeleza mpango wa Mungu kwa mwanadamu katika uhalisia wa maisha yake.

Watawa watambue kwamba, wako duniani na wanakabiliwa na athari za myumbo wa maadili ya uongozi kama inavyojionesha katika Jamii na Familia kwa ujumla. Watawa wanaalikwa kuwa ni kielelezo cha matumaini kadiri ya Mpango wa Mungu. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita ni mfano wa kuigwa aliyetambua kwamba, uongozi ni huduma. Papa Francisko anaendelea kutoa mwelekeo mpya wa uongozi kama huduma, kwa kuwa karibu zaidi na Familia ya Mungu pamoja na Watu wote wenye mapenzi mema.







All the contents on this site are copyrighted ©.