2013-05-24 11:17:11

Ziara ya kikazi ya Rais Barack Obama Barani Afrika!


Taarifa kutoka Ikulu ya Marekani inaonesha kwamba, Rais Barack Obama wa Marekani kuanzia tarehe 26 Juni hadi tarehe 3 Julai 2013 atakuwa na ziara rasmi ya kikazi Barani Afrika na atapata fursa ya kutembelea Senegal, Afrika ya Kusini na Tanzania.
Itakumbukwa kwamba, kwa mara ya kwanza Rais Obama alitembelea Ghana kunako mwaka 2009, kwa kukazia kwamba, Bara la Afrika litaendelezwa na Waafrika wenyewe! Misaada inayotolewa na Jumuiya ya Kimataifa na Wahisani mbali mbali iwe ni kikolezo cha maendeleo ya Watu wa Bara la Afrika, sanjari na kudumisha utawala bora.
Katika ziara hii, Rais Obama atapata fursa ya kukutana na viongozi wa Serikali, Wafanyabiashara na wadau mbali mbali. Ziara ya Rais Obama nchini Afrika ya Kusini, inaweza kuwa ni fursa ya pekee kwake kuweza kukutana na kuzungumza na Mzee Nelson Mandela, ambaye kwa siku za hivi karibuni afya yake imekuwa na mgogoro. Wachunguzi wa mambo wanasema, Rais Obama kwa mara ya kwanza alikutana na Mzee Madiba kunako mwaka 2005 wakati ambapo Obama alikuwa bado ni Seneta.
Ziara ya Rais Obama Barani Afrika, inasema Ikulu ya Marekani ni kuendeleza ushirikiano wa kimataifa na nchi za Kiafrika, kwa kuwekeza zaidi katika masuala ya uchumi, biashara na maendeleo endelevu ya watu hasa Kusini mwa Jangwa la Sahara, bila kusahau umuhimu wa kudimisha demokrasia na utawala wa sheria. Ni wakati muafaka kwa nchi za Kiafrika kuwekeza katika teknolojia rafiki pamoja na kuwajengea uwezo vijana ili kushiriki katika mchakato wa kujiletea maendeleo yao.
Uamuzi wa Rais Obama kutotembelea Kenya kwa mara ya pili tangu achaguliwe, kumewafanya baadhi ya wananchi wa Kenya kujiuliza maswali yasiyokuwa na majibu muafaka. Wanasema, pengine ni fursa kwa wanasiasa wa Kenya kujichunguza zaidi ili kurekebisha kasoro zinazoifanya kutengwa katika matukio kama haya.
Rais Obama kabla ya kuanza ziara yake Barani Afrika, hapo tarehe 7 hadi tarehe 8 Juni, 2013 kwa mara ya kwanza atakutana na kuzungumza na Rais Xi Jinping wa China ambaye amechaguliwa hivi karibuni. Inawezekana ziara hii ikawa ni jukwaa la kuweza kubadilishana mawazo kuhusu masuala kadhaa kati ya Ulaya na Asia kabla ya Wakuu wa G 20 kufanya mkutano wao huko Pitisburg.
Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania, Bernard Membe amesema ujio wa Rais wa Marekani Barack Obama ni wa umuhimu kwa nchi kwani utaipatia Tanzania zaidi ya dola milioni 800 (sawa na Sh. Trilioni 1.3) kwa ajili ya kukamilisha Malengo ya Maendeleo ya Milenia. Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe amesema ujio wa Rais wa Marekani Barack Obama ni wa umuhimu kwa nchi kwani utaipatia Tanzania zaidi ya dola milioni 800 (sawa na Sh. Trilioni 1.3) kwa ajili ya kukamilisha Malengo ya Maendeleo ya Milenia ifikapo mwaka 2015.
Membe alisema fedha hizo zitasaidia kukamirisha miradi mbalimbali katika sekta za barabara, maji na elimu, akiwa nchini Rais Obama ataongozana na ujumbe wa wafanyabiashara 700.








All the contents on this site are copyrighted ©.