2013-05-23 11:02:13

OAU inaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipoanzishwa!


Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika, OAU ambao kwa sasa unajulikana kama Umoja wa Afrika yameanza kutimua vumbi mjini Addis Ababa, Jumatano tarehe 22 Mei 2013 na kilele cha Maadhimisho haya ni Jumamosi, tarehe 25 Mei 2013.

OAU imetekeleza madhumuni yake kwani leo hii nchi zote Barani Afrika zimejipatia uhuru wa bendera na zinaendelea kujikwamua katika masuala ya kiuchumi, kijamii na kisiasa. Utawala wa ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini umeng'olewa, leo Afrika ya Kusini ni kitovu cha maendeleo Kusini mwa Afrika.

Katika Maadhimisho haya, Wakuu wa Umoja wa Afrika watajiwekea mikakati na maazimio kwa ajili ya utekelezaji katika kipindi cha miaka mingine 50 ijayo katika masuala ya kiuchumi, kisiasa na kijamii. Umoja wa Afrika una jumla ya wanachama 53 na umekuwa ni kiungo kikuu na sauti ya Bara la Afrika katika masuala mbali mbali. Umaskini, ujinga na magonjwa; haki, amani na maendeleo endelevu ni kati ya changamoto zinazoendelea kuzikumba nchi nyingi za Bara la Afrika.

Uzalendo ukipewa kipaumbele cha kwanza, rasilimali na utajiri uliomo Barani Afrika ukatumika kwa ajili ya mafao ya wengi, Waafrika wanaweza kucharuka katika maendeleo! Vinginevyo, Bara la Afrika litaendelea kudidimia! Viongozi mbali mbali wanashiriki katika Maadhimisho haya.







All the contents on this site are copyrighted ©.