2013-05-22 10:05:17

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anaichangamotisha Msumbiji kupambana na umaskini pamoja na magonjwa!


Umaskini wa hali na kipato na magonjwa ni kati ya changamoto kubwa zinazoikabili Msumbiji katika kipindi, hata kama kuna utashi na mikakati ya kupambana na hali hii nchini Msumbiji, kwani kuna dalili za maboresho ya hali ya kiuchumi na kijamii.

Ni maneno ya Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon mapema juma hili alipokuwa anafanya ziara ya kikazi ya siku mbili nchini Msumbiji kabla ya kujiunga na Umoja wa Afrika katika Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika ulipoanzishwa.

Msumbiji imeonesha utashi wa kisiasa na kiuchumi katika kuwaletea watu wake maendeleo endelevu mara baada ya vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo kimsingi imekuwa ni kikwazo kikubwa cha maendeleo nchini Msumbiji. Kuna dalili za maendeleo makubwa Barani Afrika yanayokwenda sanjari na uhru pamoja na utawala bora na watu wanaonesha imani kubwa kwa Afrika iliyo bora kwa siku za usoni. Msumbiji ni mfano na kielelezo cha kuigwa anasema, Bwana Ban Ki- Moon.

Hata hivyo bado kuna idadi kubwa ya wananchi wengi Barani Afrika wanaoendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini na magonjwa, changamoto ya kuweka mikakati makini katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015. Bado Umoja wa Mataifa unaonesha wasi wasi wa kuweza kufikiwa kwa Malengo haya lakini, umedhamiria kutekeleza mikakati hii ka hali na mali. Athari za mabadiliko ya tabianchi bado zinaendelea kuleta maafa makubwa sehemu mbali mbali dunia na Msumbiji imekuwa ikiathirika mara kwa mara.







All the contents on this site are copyrighted ©.