2013-05-21 07:53:57

Makanisa Barani Afrika yana mchango mkubwa katika kudumisha demokrasia na utawala bora


Baraza la Makanisa Ulimwenguni linasema, Makanisa Barani Afrika yana matumaini makubwa kwamba, Serikali zitaweza kuendeleza mchakato wa utawala bora, misingi ya haki, amani, demokrasia na utulivu kama kikolezo cha maendeleo endelevu ya binadamu kiroho na kimwili.

Hivi karibuni, wawakilishi wa Makanisa, Vyama vya Kiekumene pamoja na Vyama vya kiraia walikusanyika nchini Zimbabwe ili kupembua kwa kina na mapana mchango wa Makanisa katika kudumisha haki, amani, utulivu, utawala wa sheria na demokrasi ya kweli Barani Afrika, kwa kuzingatia kwamba, katika miezi ya hivi karibuni kuna nchi kadhaa Barani Afrika zitakuwa zinafanya uchaguzi mkuu, Zimbabwe ni kati ya nchi hizi.

Kwa pamoja wajumbe wamekazia umuhimu wa kuwa na Serikali imara itakayosimamia kwa ukamilifu maendeleo ya wananchi wake badala ya kuendekeza migogoro na kinzani ambayo imekuwa ni chanzo cha wananchi kukata tamaa na mkwamo wa maendeleo ya watu katika sekta mbali mbali za maisha. Viongozi wa Makanisa wanasema, Kanisa linaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kwa Jamii kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza nchini Zimbabwe.

Wananchi wa Bara la Afrika hawana budi kushirikiana kwa pamoja katika kujenga na kudumisha misingi ya demokrasia na utawala bora kama sehemu ya mchakato wa kuimarisha haki na amani Barani Afrika. Kutokana na ukweli huu, Makanisa hayana budi kushirikiana kwa pamoja katika kutafuta na kudumisha mafao ya wengi; pamoja na kuhakikisha kwamba, uongozi unakuwa ni kwa ajili ya huduma kwa raia.

Kipindi cha mpito kuelekea kwenye demokrasi ya kweli, hakina budi kupewa kipaumbele cha pekee kwani hapa kwa miaka mingi pamekuwa ni chanzo cha vurugu, vita na kinzani za kijamii. Kwa hakika mchango wa Makanisa unafahamika katika harakati za ukombozi Barani Afrika. Changamoto kwa Makanisa kwa wakati huu ni kuhakikisha kwamba, yanakuwa ni vyombo vinavyowaunganisha watu kwa ajili ya mafao, ustawi na maendeleo yao: kiroho na kimwili na kwamba, kila mwananchi ana haki ya kushiriki katika kudumisha demokrasia na utawala bora.







All the contents on this site are copyrighted ©.