Watumishi wa Serikali ya Tanzania kupata mikopo ya nyumba kuanzia Septemba, 2013.
Watumishi wa Serikali, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, kuanzia Septemba
mwaka huu wataanza kunufaika na mikopo nafuu ya ujenzi wa nyumba za kuishi chini ya
utaratibu mpya ulioandaliwa na Serikali na unaojulikana kama Mpango Maalum wa Nyumba
za Kuishi za Watumishi wa Umma – Public Servant Housing Scheme.
Mpango huo
ulitangazwa , Ijumaa, Mei 17, 2013 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete wakati wa hotuba yake ya kufunga Wiki ya Mifuko ya Hifadhi ya
Jamii kwenye bustani ya Nyerere Square mjini Dodoma.
Hata kabla ya kuutangaza
Mradi huo hadharani mjini Dodoma, Rais Kikwete alikwishakuambiwa na Gavana wa Benki
Kuu ya Tanzania, Profesa Beno Ndullu kuwa chini ya Mpango huo, watumishi wa Serikali
kuanzia Septemba mwaka huu wataweza ama kukopa nyumba za gharama nafuu ama kukopa
mikopo ya gharama nafuu ambayo italipwa katika kipindi cha miaka 25.
Gavana
Ndullu alikuwa Mwenyekiti wa Kamati Maalum iliyoteuliwa na Rais Kikwete kuangalia
jinsi gani ya kuwasaidia watumishi wa Serikali katika Tanzania kuweza kupata mikopo
nafuu ama kukopa nyumba za bei nafuu ambayo iliwasilisha ripoti yake kwake katika
mkutano uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam katikati ya wiki iliyopita.
Chini
ya mpango huo, ambao utaendeshwa na kampuni iitwayo Watumishi Housing Company Limited
iliyoandikishwa na kupewa usajili Februari mwaka huu, 2013, kiasi cha nyumba 5,000
zitajengwa katika miaka ya kwanza mitano, mwaka wa kwanza zikiwa zimejengwa nyumba
2,500.
Mpaka sasa kiasi cha Sh. bilioni 68 zimekwishapatikana kati ya kiasi
cha Sh.bilioni 358 zinazotarajiwa kuwekezwa katika Mradi huo katika miaka hiyo mitano
ya mwanzo na itakuwa ni kampuni hiyo ambayo itajenga nyumba za gharama nafuu na kuwezesha
kupatikana kwa mikopo nafuu kwa watumishi ambao watapendelea kukopa fedha ili kujenga
wenyewe nyumba za kuishi.
Taasisi zitakazoshiriki katika kampuni hiyo ni pamoja
na mifuko ya Hifadhi ya jamii ya NSSF, PPF, PSPF, LAPF, GEPF, Shirika la Nyumba la
Taifa (NHC) pamoja na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).
Mbali na taasisi
hizo, pia benki 10 zimekubali kushiriki katika Mradi huo. Mabenki hayo ambayo yatakuwa
yanatoza riba ya kati ya asilimia 10 na 13 kwa miaka yote 25 ya mkopo ni NMB, CRDB,
NBC, Bank of Africa, Azania Bank, EXIM Bank, Banc ABC, NIC Bank, DCB Bank na KCB.