2013-05-20 14:09:44

Askofu mkuu Justin Portal Welby akutana na kuzungumza na Rais Kikwete, mjini Dodoma


Rais Jakaya Mrisho Kikwete Jumamosi, Mei 18, 2013, amekutana na kufanya mazungumzo na Kiongozi wa Kanisa Anglikana Duniani, Askofu Mkuu Justin Portal Welby wa Jimbo kuu la Cantebury, Uingereza ambaye pia ni mkuu wa Kanisa Anglikana Duniani.

Katika mkutano huo uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Mt. Gaspar mjini Dodoma, Rais Kikwete amemshukuru sana Askofu Mkuu kwa mchango wa Kanisa Anglikana katika maendeleo ya Tanzania katika nyanja za elimu, afya na masuala mengine ya jamii na uwezeshaji wa wananchi.

Viongozi hao wawili walikuwa mjini Dodoma kushiriki katika sherehe za kutawazwa kwa Askofu Dkt. Jacob Erasto Chimeledya kuwa Askofu Mkuu na Kiongozi wa sita wa Kanisa Anglikana Tanzania. Sherehe hizo zimefanyika katika Kanisa Kuu la Kanisa Anglikana la Roho Mtakatifu mjini Dodoma na kuhudhuriwa na maelfu kwa maelfu ya wananchi.

Rais Kikwete pia amemshukuru Askofu Mkuu Welby kwa uamuzi wake wa kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza duniani kuitembelea na kushiriki katika sherehe za kusimika askofu tokea kuteuliwa kushika nafasi hiyo kubwa ya ukuu wa Kanisa la Anglikana duniani Machi mwaka huu.

Askofu Mkuu Welby amemwambia Rais Kikwete kuwa ni furaha kubwa kwake kuja Tanzania ikiwa ni mara ya tatu kuitembelea nchi hii katika maisha yake. Alikuja Tanzania kwa mara ya kwanza mwaka 1974 na baadaye mwaka 1996. “Nimefurahi sana kuja tena Tanzania na nakuhakikishia kuwa Tanzania, Watanzania na wewe Mheshimiwa Rais mnabakia katika sala zetu na kumbukumbu zetu daima,” amesema Askofu Mkuu Welby.








All the contents on this site are copyrighted ©.