2013-05-19 11:11:24

Umewekwa wakfu ili kuwahudumia watawa wenzako!


Mtakatifu Francisko wa Assisi alikuwa anawahimiza wafuasi wake kutangaza Injili ya Kristo, lakini zaidi wao wenyewe kuwa ni kielelezo na ushuhuda wa Injili Hai katika maisha ya watu wanaowazunguka.

Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumweka wakfu Padre Josè Rodriguez Carballo kuwa Askofu mkuu na Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Ibada ambayo imefanyika kwenye Kanisa kuu la Yakobo Mtume, Santiago di Compostella, nchini Hispania, wakati wa Kesha la Siku kuu ya Pentekoste.

Askofu mkuu Carballo anaalikwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, maisha yake yanafanana na Injili anayoitangaza, kama kielelezo cha maisha ya Kristo anayeishi na kutenda ndani mwake. Kardinali Bertone, amemtaka Askofu mkuu Carballo anapotekeleza utume wake, kuendelea kuhimiza umuhimu wa watawa kuwa waaminifu kwa karama na maisha yao, daima wakijitahidi kusoma alama za nyakati ili kujibu kilio cha watu wa nyakati hizi. Watawa wanao mchango mkubwa katika kumhudumia mwanadamu wa leo, wakiwa na shukrani kwa maisha yaliyopita na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi.

Kwa namna ya pekee, Kardinali Bertone amemtaka Askofu mkuu carballo kuwa mwaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, changamoto endelevu kwa viongozi waliopewa dhamana katika Kanisa na Jamii kwa ujumla wake. Kama Askofu mkuu anapaswa kuwa mwaminifu kwa Mafundisho ya Mitume, daima akijitahidi kushikamana na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa njia ya maisha na mafundisho yake.

Ametakiwa kuwa mwaminifu kwa karama ambazo Mwenyezi Mungu amemkirimia katika maisha na ambazo anapaswa kuzipyaisha kila siku ya maisha yake. Lakini zawadi kubwa aliyopewa na Mwenyezi Mungu ni utawa kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa la Kristo.

Askofu Mkuu Carballo ametakiwa kuwa mnyenyekevu katika kutafuta na kuuishi ukweli ambao ni Kristo mwenyewe, kwa njia hii atamwezesha kuwa mkweli na mwaminifu katika maisha na wito wake. Aendelee kuwa ni mtumishi mwaminifu kwa Mungu na jirani, jambo linalorutubishwa kwa Sakramenti, Sala na Tafakari ya Neno la Mungu. Ameombewa Mapaji ya Roho Mtakatifu wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Siku kuu ya Pentekoste.







All the contents on this site are copyrighted ©.