2013-05-19 09:53:43

Shuhuda kwa baadhi ya waamini wakati wa Kesha la Pentekoste, Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican


Wanachama wa vyama na mashirika ya kitume mara baada ya kukiri imani yao kwenye kaburi la Mtakatifu Petro kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, majira ya mchana walikusanyika kusali na kushirikishana ushuhuda wa maisha ya kikristo kutoka katika vyama na mashirika yao. Waamini waliobahatika kutoa ushuhuda wamegusia kwa namna ya pekee imani ya kweli inavyodhihirisha upendo wa Mungu hata katika shida na mahangaiko ya ndani.

Tabu na mateso wanayoyapata watoto kwenye familia ambazo wazazi wametengana. Ni watu ambao wanakosa furaha na amani ya ndani, kiasi cha kujisikia watupu mbele ya jirani zao. Lakini, siku ile walipogundua ukweli kuhusu Fumbo la Msalaba, wakapata amani na utulivu wa ndani, kiasi cha kumkimbilia Mwenyezi Mungu ambaye amewaonjesha siri ya mafanikio katika maisha, kiasi cha kujitoa kwa ajili ya upendo kwa Mungu na jirani.
Baadhi ya waamini wamesema kwamba, walikwenda kufunga ndoa Kanisani kwa kuwafurahisha ndugu na jamaa, lakini moyoni mwao walibaki kuwa wakavu. Semina ya ndoa haikuwasaidia sana kufahamu umuhimu wa Sakramenti ya Ndoa katika hija ya maisha yao ya kiimani. Baada ya kubahatika kupata watoto wawili, walianza kuonja ugumu na utupu wa maisha.
Mafanikio waliyopata kazini, kwenye michezo pamoja na kuwa na marafiki wengi, hayakuwaletea nafuu katika utupu wao wa ndani. Walitamani kupata mtoto wa tatu, lakini haikuwezekana kutokana na matatizo waliyokumbana nayo kiasi cha kutupiana maneno makali na hatimaye, kuachana. Pendo walilokuwa wamelianzisha wakiwa na umri wa miaka 23 likaingia mchanga.
Wote wawili wakakosa raha, amani na utulivu wa ndani. Wakaanza mchakato wa kutalakiana, lakini baadaye wakagundua kwamba, bado walikuwa wanapendana kwa dhati licha ya mapungufu yaliyojitokeza katika hija ya maisha yao kama wanandoa. Katika kipindi cha mahangaiko yote haya, alianza hija ya imani na wakasaidiwa na wanachama wenzao kugundua tena ile furaha ya imani katika upendo.
Tarehe 14 Septemba 2011 wakakutana tena nyumbani kwao na kuanza maisha wakitambua kwamba, kukosa na kukoseana ni sehemu ya maisha, kusamehe na kusahau ni kuanza hija ya utakatifu. Leo hii wanaadhimisha Jubilee ya miaka 25 ya maisha yao ya ndoa!
Kijana mmoja amesema kwamba, hakuwa amebatizwa wala kufunga ndoa. Kwake maisha yalikuwa ni sawa na ”kuku kwa mrija” Alioa na kubahatika kupata mtoto. Wakati wa maandalizi ya ubatizo wa mtoto wao, huo ukawa ni mwanzo wa mchakato wa wongofu wa kumtafuta Yesu. Akawa na hamu ya kusoma na kutafakari Maandiko Matakatifu; akaanza kushiriki katika Misa Takatifu pamoja kuwamegea wengine upendo uliokuwa unabubujika kutoka katika imani yake kwa Kristo na Kanisa lake. Kunako mwaka 2012 wakati wa Siku kuu ya Pasaka, akabatizwa, anamshukuru Mungu kwa wema na ukarimu wake.
Kuna kijana mmoja amesema kwamba, katika maisha yake amekumbana na nyakati za giza na utupu wa maisha, lakini alipokutana na Yesu Mfufuka amemwezesha kupata ari na mwamko mpya, katika maisha na utume wake ndani ya Kanisa. Tangu wakati huo, amekuwa ni kijana anayejihusisha na shughuli za kijamii kwa kuwaonjesha wengine ile furaha ya kumwamini Kristo.
Wanandoa wapya, wao walipata mwaliko wa kushiriki katika maisha ya sala kama njia ya kuchangia mchakato wa Uinjilishaji mpya, kwa njia hii wamekuwa na kukomaa katika maisha na utume wa Kanisa baada ya kuanza hija ya toba na wongofu wa ndani hatua kwa hatua.
Mwanafunzi mmoja kutoka Chuo Kikuu cha Bicocca Milano, Italia anasema, maisha ya sala na tafakari ya Neno la Mungu yamemchangamotisha kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya jirani zake katika huduma ya afya. Hivi ndivyo ilivyokuwa hata kwa Mkurugenzi wa afya ambaye kunako mwaka 1995 alijiunga na Chama cha kitume, tangu wakati huo amekuwa na mwelekeo mpya kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Hii ikawa ni dira na mwelekeo wake wa Kimissionari.
Baadhi ya waamini waliotoa ushuhuda wao mbele ya Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican wamekiri kwamba, familia imekuwa chemchemi ya imani katika hija ya maisha yao kwa Kristo na Kanisa lake. Imani hii imerutubishwa kwa njia ya ushuhuda kutoka kwa wazazi na majirani ambao wamekuwa kweli ni mfano bora wa kuigwa. Kwa sasa ana amini na anamwomba Yesu amwongezee imani.








All the contents on this site are copyrighted ©.