2013-05-19 11:23:58

Roho Mtakatifu ni mhimili wa maisha na utume wa Kanisa Ulimwenguni!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Sherehe ya Pentekoste, ambayo kwa Mwaka wa Imani imekuwa pia ni fursa kwa vyama na mashirika ya kitume kutoka sehemu mbali mbali za dunia kusali pamoja na kutafakari Neno la Mungu, tayari kwenda hadi miisho ya dunia ili kumtangaza na kumshuhudia Kristo kwa njia ya maisha yao. Kwa njia ya Roho Mtakatifu Kanisa liliweza kuenea sehemu mbali mbali za dunia.

Mitume pamoja na Bikira Maria walipokuwa wamekusanyika kwenye Chumba cha juu walijazwa na nguvu ya Roho Mtakatifu katika undani wao, yaani katika akili na mioyo yao kiasi cha kuanza kuzungumza kwa lugha mbali mbali kadiri Roho wa Bwana alivyowawezesha. Haya ni matendo makuu ya Mungu yaliyowashangaza hata wale waliokuwepo kwenye eneo la tukio.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake anapembua mambo makuu matatu: upya, utulivu na utume ambao Mama Kanisa amekabidhiwa kuuendeleza. Upya anasema Baba Mtakatifu ni dhana inayomwezesha mtu kuwa na uhakika wa usalama wa maisha yake, hali ambayo wakati mwingine inajitokeza katika maisha ya kiroho. Si rahisi kwa mwamini kujiamisha moja kwa moja kwa Mwenyezi Mungu na kumwachia nafasi roho Mtakatifu ili aweze kuwaongoza katika maisha na maamuzi yao. Mwanadamu anaogopa njia mpya ambayo anaweza kuoneshwa na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yake. Kutokana na ubinafsi, mwanadamu anajikuta akijifunga ndani mwake.

Lakini Mwenyezi Mungu katika Historia ya Wokovu, amejifunua na kumletea mwanadamu mabadiliko ya ndani, kama inavyojionesha katika maisha ya Mababu wa Imani, hadi Siku ya Pentekoste, Roho Mtakatifu alipowashukia Mitume, wakapata ujasiri wa kutoka kifua bele kumtangaza Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Upya huu ni utimilifu wa furaha, amani na utulivu wa ndani kwani Mwenyezi Mungu anawatakia watu wake mema.

Baba Mtakatifu anawauliza waamini ikiwa kama wako wazi kupokea maajabu ya Mungu katika hija ya maisha yao? Au wanaelemewa na woga na wasi wasi wa uwepo wa Roho Mtakatifu? Je, waamini wako tayari kuanza kutembea katika njia mpya ambayo Mwenyezi Mungu amewaandalia katika hija ya maisha yao?

Baba Mtakatifu anasema, Roho Mtakatifu ni msingi wa amani na utulivu ndani ya Kanisa. Anawajalia waamini karama na mapaji mbali mbali ili kujenga na kuimarisha umoja, kwani Yeye ni kielelezo cha Umoja katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Umoja huu unaojionesha kwa namna ya pekee katika utofauti, kwani hapo waamini wanatambua nafasi na dhamana ya Roho Mtakatifu ambaye anawachangamotisha kujenga na kuimarisha umoja wa Kanisa.

Waamini wanapofanya hija huku wakishikamana na viongozi wao, ambao wamekirimiwa karama na utume hizi ni dalili kwamba, wanaongozwa na Roho Mtakatifu. Umoja na mshikamano wa Kanisa ni jambo msingi kwa kila mwamini, chama na shirika la kitume. Ni kwa njia ya Kanisa kwamba, wanaweza kukutana, kumfahamu na kufahamiana na Kristo. Huu ni mwaliko kwa vyama na mashirika ya kitume kuhakikisha kwamba, daima yanafuata Mafundisho ya Kanisa ili kuendelea kushikamana na Yesu Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko akizungumzia kuhusu utume wa Kanisa anakazia kwamba, Roho Mtakatifu anawawezesha waamini kulifahamu Fumbo la Mungu aliye hai, anayewasukuma kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutangaza na kutolea ushuhuda wa Habari Njema ya Wokovu; wanatumwa kuwashirikisha wengine ile furaha ya imani baada ya kukutana na Yesu Kristo katika hija ya maisha yao!

Roho Mtakatifu ni mhimili wa utume wa Kanisa, changamoto ya kuendeleza utume wa Kanisa uliojionesha kwa mara ya kwanza yapata miaka elfu mbili iliyopita. Roho Mtakatifu ni zawadi ya hali ya juu kabisa kutoka kwa Kristo Mfufuka, inayopaswa kumfikia kila mwanadamu. Roho Mtakatifu ni Mfariji anayewapatia waamini ujasiri wa kumtangaza Kristo, mwaliko kwa waamini kuendelea kujishikamanisha na Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko amehitimisha mahubiri yake kwa kuwakumbusha waamini kwamba, Liturujia ya Sherehe ya Pentekoste ni Sala ya Kanisa linaloungana na Kristo ili kumwomba Mwenyezi Mungu aendelee kuwakirimia Roho Mtakatifu, ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa Kanisa. Kanisa linaungana na Bikira Maria kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze kuwajaza waamini na ule moto wa mapendo.







All the contents on this site are copyrighted ©.