2013-05-18 11:50:01

Wambeya hawana Bunge!


Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kujishughulisha zaidi na maisha yao ya Kikristo badala ya kupoteza muda mrefu wa kupiga soga zisizo na tija, mafao wala maendeleo yao kiroho na kimwili kwao na kwa jirani zao na matokeo yake ni kupoteza wakati na dira ya maisha.

Baba Mtakatifu ameyasema hayo Jumamosi, tarehe 18 Mei 2013 wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican. Baba Mtakatifu anasema, kuna kishawishi cha watu kutaka kuingilia mambo ya jirani zao wakati ya kwao wenyewe yanawashinda, hali ambayo wakati mwingine inajenga wivu na uhasama usiokuwa na tija wala mashiko kwa watu!

Kishawishi hiki kinaweza kukua na kupanuka hata kufikia katika ngazi ya Kanisa, kumbe kuna haja kwa waamini kuwa macho na makini kwani, maseng'enyo yanahribu sifa ya jirani. Waamini wajifunze kuzungumza na kusimamia ukweli badala ya kuchafua majina ya jirani na ndugu zao kama njia ya kujipatia sifa uchwara! Anakumbusha kwamba, kusema uongo ni dhambi, jambo ambalo Yesu mwenyewe alilikemea kwa kumtaka Mtakatifu Petro kujishikamanisha zaidi na Yeye badala ya kupoteza mwelekeo katika njia ya wokovu.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kufuata nyayo za Kristo katika hija ya maisha yao ya kila siku, huku wakiomba neema na baraka za kutembea na kuishi katika maisha manyofu bila kupoteza dira na mwelekeo wa maisha. Wakristo wajifunze kumpenda na kumtumikia Yesu na Kanisa lake, kila mtu kadiri ya karama, nafasi na uwezo aliokirimiwa na Roho Mtakatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.