2013-05-17 08:22:46

Madhehebu ya Kipentekoste na changamoto zake!


Idadi ya Wakristo wa Madhehebu ya Kipentekoste inazidi kuongezeka maradufu duniani. Kunako mwaka 2000 kulikuwa na waamini millioni 582, idadi hii inatarajiwa kuongezeka hadi kufikia waamini millioni 800 ifikapo mwaka 2025 kadiri ya tafiti zilizofanywa na Kituo kimoja cha Utafiti kutoka Marekani. RealAudioMP3
Haya ni madhehebu yanayojikita katika imani na maisha ya kijamii. Hii ni changamoto kubwa kwa Kanisa Katoliki hasa Barani Afrika na Amerika ya Kusini.
Ni maneno ya Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo wakati akichangia mada kwenye Kongamano la Kiekumene lililoandaliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Ujerumani na kufanyika mjini Roma hivi karibuni. Wachunguzi wa masuala ya kidini kimataifa wanaendelea kufanya utafiti ili kubaini ni mambo yepi ambayo yamepelekea kiasi kwamba, Madhehebu ya Kipentekoste kuendelea kustawi na kushamiri Barani Afrika na Amerika ya Kusini katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni.
Vikundi hivi vya kidini vinaendelea kupata wafuasi wengi pembezoni mwa miji mikuu; maeneo yanayokaliwa na watu wanaokimbia kutoka vijijini wakitafuta fursa za ajira na unafuu wa maisha. Haya ni maeneo ambayo yanakabiliwa na umaskini mkubwa kiasi kwamba, watu wanaoishi katika mazingira kama haya wanajisikia kuwa wageni hata katika nchi zao wenyewe.
Viongozi wa Madhehebu ya Kipentekoste wamekuwa ni mfano bora wa kuigwa, kwani wanawaonjesha moyo wa ukarimu na kuwapatia huduma msingi za maisha ya kiroho na kimwili kiasi kwamba, wanajisikia wako nyumbani.
Haya ndiyo yanayojitokeza nchini Brazil na kwenye baadhi ya nchi za Kiafrika. Madhehebu haya yamekuwa ni kimbilio la watu wengi waliokata tamaa, wenye shida na mahangaiko ya ndani; watu wanaohitaji faraja na kuthaminiwa. Ni Madhehebu yanayojitambulisha kama Familia inayojali watu wake; hapan i mahali ambapo wanafamilia wanasaidiana wakati wa raha na shida ili kuweza kufikia malengo ya maisha hasa katika kukabiliana na hali ngumu ya maisha na umaskini ambao kwa sasa ni tatizo na changamoto kwa wengi.
Kuna baadhi ya Waamini wanatafuta miujiza katika maisha baada ya kukabiliana na magumu mbali mbali: ikiwa ni pamoja na magonjwa, ukata, ukahaba, matumizi haramu ya dawa za kulevya na shida nyingine za maisha kama vile imani za kishirikina na mapepo wachafu. Wakifika huko, kila mmoja wao anaahidiwa kupata muujiza wake kutoka kwa Yesu! Huu ni mfumo ambao unajionesha hata katika Makanisa na Jumuiya za Kikristo.
Karl Gabriel kutoka Chuo Kikuu cha Munster, Ujerumani anabainisha kwamba, kuna baadhi ya watu walidhani kwamba, Makanisa ya Kipentekoste yangeweza kufutika kwenye uso wa dunia, lakini kinyume chake ni kwamba, yanaendelea kushamiri na kustawi kama mtende wa Lebanoni. Kukua na kuenea kwa Ukristo sehemu mbali mbali za dunia ni mchango mkubwa unaotolewa na vikundi hivi kama inavyojionesha Amerika ya Kusini, Kusini mwa Afrika na baadhi ya nchi za Asia bila kusahau China. Hapa waamini wanajisikia kuwa ni sehemu ya Kanisa na wala si wapita njia.
Wachunguzi wa masuala haya wanasema kwamba, idadi ya wafuasi wa Madhehebu ya Kipentekoste ni wanawake, wanaovutwa kwa urahisi zaidi na ushawishi unaotolewa na Madhehebu haya hasa kutokana na hali duni ya maisha wanayokabiliana nayo. Uduni wa maisha unaweza kuwa ni ukata wa fedha au pia umaskini wa maisha ya kiroho!
Monsinyo Juan Fernando Usma Gòmez kutoka Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo anasema kwamba, hii ni kati ya changamoto kubwa zinazoyakabili Mabaraza ya Maaskofu Katoliki sehemu mbali mbali za dunia kutokana na ukweli kwamba, ni hali inayogusa undani wa maisha ya Kanisa.
Hii pia ni changamoto kubwa katika mchakato wa majadiliaano ya Kiekumene, kwani hawa pia wanapaswa kushirikishwa kama wadau wapya, Kanisa linapojitahidi kutafuta umoja miongoni mwa watoto wake waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia. Hili si jambo rahisi hata kidogo; ukweli na unyenyekevu vinapaswa kutawala hapa.
Kardinali Kurt Koch anasema swali la msingi ambalo Kanisa Katoliki linapaswa kujiuliza ni kwa nini Wakatoliki wanashawishika kwa urahisi kuingia kwenye Mashehebu ya Kipentekoste? Kuna haja ya kuangalia hali ya Ukristo katika ngazi ya Ulimwengu kwa ujumla na katika nchi husika. Kwa kutambua: matatizo, fursa na changamoto zilizopo, hapo Mabaraza ya Maaskofu Katoliki yatafute mbinu mkakati utakaowawezesha kujikita zaidi katika mchakato wa umissionari kwa kuangalia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Wawe ni mashahidi wa kile wanacho amini na kutenda kiasi kwamba, imani yao ijioneshe katika matendo halisi, ya ukweli na wema.
Imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP. S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, kwa msaada wa Gazeti la L’Osservatore Romano.








All the contents on this site are copyrighted ©.