2013-05-15 07:34:01

Familia ni Habari Njema Duniani


Maadhimisho ya Siku ya Saba ya Familia Kimataifa yaliyofanyika Jimbo kuu la Milano, Kaskazini mwa Italia kunako mwaka 2012 yaliongozwa na kauli mbiu: Familia, Kazi na Sherehe. Maadhimisho ya Nane ya Siku ya Familia Kimataifa yatakayoanza kutimua vumbi kuanzia tarehe 22 hadi 27 Septemba 2015 Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani, yataongozwa na kauli mbiu “Familia ni Habari Njema Duniani”.

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika maadhimisho ya Juma la 47 la Maisha ya Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Italia, litaongozwa na kauli mbiu “Familia, matumaini na ujio wa Jamii ya Waitaliani.” Familia haina budi kufahamika kwamba, ni rasilimali nyeti katika Jamii na kielelezo cha uchumi makini ambao kimsingi ni nguzo imara ya sera bora na majadiliano ya kitamaduni.

Hayo ndiyo yaliyoibuliwa hivi karibuni wakati wa mwendelezo wa mikutano inayopania kukoleza majiundo ya kifamilia inayoendeshwa na Baraza la Kipapa la Familia kama sehemu ya mchakato wa kuwekeza katika Familia ili ziweze kusimama kidete kulinda na kutetea dhamana na wajibu wake ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.

Hivi karibuni, Askofu mkuu Vincenzo Paglia alisema, kwa mara ya kwanza katika historia ya maisha ya mwanadamu, familia katika miaka ya hivi karibuni imeandamwa kwa makombora kutoka katika medani mbali mbali za maisha. Hali hii ni changamoto kwa Kanisa kushirikiana na kushikamana na wadau mbali mbali, ili kwa pamoja waweze kutoa majibu makini kuhusu familia na dhamana yake ndani ya Jamii.

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, familia kwa uhakika haina budi kuwa ni kiini cha mikakati na sera za kichungaji kwa upande wa Kanisa. Wanasiasa, wachumi na wanazuoni wanapaswa pia kutoa mchango utakaosaidia kuenzi na kuboresha tunu msingi za maisha ya kifamilia.

Hii ni changamoto inayotolewa na Professa Stefano Zamagni kutoka Chuo Kikuu cha Bologna. Katika masuala ya uchumi, kuna sera za soko huria, uchumi jamii pamoja na uchumi ya kiraia unaokwenda sanjari na Mafundisho Jamii ya Kanisa kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu, familia pamoja na mahitaji msingi.

Hawa wanapaswa kuangaliwa kama nguvu kazi na mtaji muhimu sana katika mchakato wa maendeleo endelevu. Ili kutekeleza dhamana hii, familia haina budi kuwezeshwa kwa njia ya huduma bora za elimu na afya pamoja na kuwajali wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Familia ni rasilimali kubwa katika kukuza na kuendeleza uchumi wa Jamii yoyote, jambo ambalo wakati mwingine linasahuliwa na watunga sera, kiasi kwamba, Familia zimekuwa zinaendelea kukabiliana na kinzani, matatizo na changamoto kutoka katika medani mbali bali za maisha.

Watunga sera wanahamasishwa kuwekeza zaidi katika tunu msingi za maisha ya kifamilia, ili kuendeleza mikakati ya kufufua uchumi duniani, vinginevyo, litania ya athari za myumbo wa uchumi kimataifa itaendelea kuwa ni wimbo usiokuwa na msikilizaji!








All the contents on this site are copyrighted ©.