2013-05-14 09:51:12

Hofu ya uchaguzi mkuu nchini Nigeria kwa mwaka 2015 inaifanya Serikali kushindwa kudhibiti Kikundi cha Boko Haram!


Askofu Stephen Dami Mamza wa Jimbo Katoliki la Yola, Nigeria anasema, Serikali ya Nigeria imeshindwa kudhibiti vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na Kikundi cha Boko Haram kwa kuhofia kunyimwa kura wakati wa uchaguzi mkuu ujao. Kumekuwepo na waamini wenye misimamo mikali ya kiimani pamoja na vikundi vya kigaidi, lakini Serikali imeendelea kuwafumbia macho, kiasi hata cha kuhatarisha usalama wa raia na mali zao.

Hili ni jambo ambalo haliwezi kukubalika kwa Serikali kushindwa kudhibiti vitendo vya kigaidi nchini Nigeria kwa kuhofia kunyimwa kura na wananchi wanaounga mkono kikundi cha Boko Haram. Askofu Stephen Dami Mamza ameyasema hayo hivi karibuni wakati alipokuwa anazungumza na baadhi ya wajumbe kutoka katika Shirika la Kipapa la Makanisa Hitaji lililotembelea Jimboni mwake hivi karibuni.

Kikundi cha Boko Haram kinaendelea kusababisha maafa makubwa kana kwamba, hakuna Serikali wala vyombo vya ulinzi na usalama. Hali ni mbaya zaidi maeneo ya vijijini. Nigeria inajiandaa kufanya uchaguzi mkuu wa Rais na Wabunge ifikapo mwaka 2015.







All the contents on this site are copyrighted ©.