Serikali ya Tanzania kula sahani moja na wachochezi wa kidini?
Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema Serikali ina kazi kubwa ya kushughulika
na kundi dogo linalojihusisha na lugha za uchochezi wa kidini ambao unachangia kudhoofisha
amani ya nchi.
“Tunajua nia yao ni kufanya nchi isitawalike lakini sisi tumesema
hatukubali. Tumekubaliana na Waziri wa Mambo ya Ndani, ulinzi uimarishwe kila mahali,
mshingae kuona watu wanawahoji lakini nia njema, ya kurudisha amani yetu,” alisema
Waziri Mkuu.
Ametoa kauli Ijumaa, Mei 10, 2013 wakati akiwasilisha salamu za
rambirambi kwa niaba ya Serikali wakati wa ibada ya mazishi ya waumini watatu wa Kanisa
la Mt. Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, jijini Arusha waliofariki dunia kutokana
na mlipuko wa mabomu uliotokea Jumapili iliyopita, Mei 5, mwaka huu kanisani hapo.
Waziri
Mkuu amewaomba wanachi kutoka ushirikiano kwa vyombo vya dola kwa kutoa taarifa zozote
zitakazosaidia kwenye upelelezi wa tukio hilo.
“Ninawaomba Watanzania tushirikiane
kuwafichua watu hawa waovu kwa sababu tunaishi nao, ni watu ambao wako miongoni mwetu...
Tusaidieni kutunong’oneza ili tuchukue hatua, alisema.
Waziri Mkuu alisema
yeye ni miongoni mwa watu wanaoamini kwamba ukristo au uislamu hauwezi kuondolewa
kwa kuwaua viongozi wa dini au waumini wao. “Ni kujidanganya tu mtu akiamini kuwa
akimuua Askofu, Mufti au Mwamini ataimaliza dini yoyote. Madhehebu haya mawili ni
nguzo kubwa kwa Taifa letu, tunatamani tuendelee kuwa na amani iliyokuwepo siku zote,”
alisisistiza.
Alisema Serikali kupitia idara ya maafa itatoa sh. milioni 100/-
ili zisaidie kukabiliana na janga lililowakabili wana Arusha.
Mapema, akiongoza
ibada hiyo, Kardinali Polycarp Pengo aliwataka waamini wote kutolipa uovu kwa uovu
bali watende wema ili kusahihisha maovu. “Ishara ya uovu imetendwa na hawa watu dhidi
ya waumini wenzetu kwa madhumuni yanayojulikana na wao tu bila kuchokozwa na hawa
marehemu ama wale waliko hospitali (majeruhi),” alisema.
“Uovu umeshatendwa,
Je, sisi tufanye nini? Angekuja hapa Kanisani yule aliyesababisha mauti haya, tungemfanya
nini?” Alihoji Kardinali Pengo na kujibiwa na mamia ya waumini waliohudhuria ibada
hiyo: “Tungemsamehe.”
Aliwasihi waamini wote kuendelea kuliombea Taifa la Tanzania
ili tukio hilo na lile la kuuawa kwa Padre Evarist Mushi kule Zanzibar yasiwe sababu
ya kusambaratika kwa amani ya Taifa hili.
“Tusilipe ubaya kwa ubaya, tuendelee
kuomba Mungu asikie sala yetu na awazindue wenye mamlaka watimize wajibu wao,” alisema.
Naye
Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk. Alex Malasusa
akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF), alilaani
waliosababisha mauaji hayo na kusema kitendo hicho kimelitia doa Taifa kwa vile ni
kitendo kinachoashiria kuchafua amani ya Tanzania.
Aliwasihi waumini wote kutokuwa
waona katika kazi ya kumtanga za Kristo. “Risasi zinapigwa, mioto inayowashwa katika
makanisa yetu na mabomu yanayolipuliwa yasiwe sababu ya kututia hofu. Imani yetu haiko
katika miili bali iko mioyoni mwetu,” alisema.
Askofu Mkuu Josephat Lebulu
wa Jimbo Kuu la Arusha akitoa shukrani kwa niaba ya Kanisa Katoliki aliwashukuru wote
waliofika kuwafariji kutokana na tukio hilo na kuwathibitishia kuwa kama Kanisa wameguswa
na moyo waliouonyesha.
“Tupige goti, ndiyo kazi tuliyonayo. Tupige goti ili
Mungu awafichue hawa watu, aufichue mfumo wao wa kiovu, na awape nguvu viongozi wetu
wao ni kama sisi na iko siku watatoa hesabu mbele ya Mwenyezi Mungu,” alisema.
Aliwasihi
waumini wote kutoogopa na kuendelea kuomba ili waliohusika na uovu huo Mungu awafichue
na kuwaonyesha hadharani. “Ninaambiwa msiogope, hakuna kutishwa kwa namna yoyote tunaposimama
na Kristo... sisi hatupaswi kuogopa kwa sababu Kristo alishinda mauti,” alisisitiza.
Watu
66 waliathirika kutokana na mlipuko huo uliotokea Mei 5, mwaka huu ambapo watatu wamefariki
dunia na kati ya wagonjwa 63 waliobakia, wanane walihamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili,
wengine waliotibiwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani, na baadhi wanaendelea kupatiwa
matibabu mjini Arusha.