2013-05-11 09:53:40

Mwambieni Mwenyezi Mungu IMETOSHA!


Mahubiri ya Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam wakati wa Ibada ya Misa ya Mazishi ya waamini watatu waliofariki kwa kulipuliwa na bomu, Jumapili tarehe 5 Mei 2013 pamoja na kufungua rasmi Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi Olasiti, Jimbo kuu la Arusha, Tanzania, tukio ambalo lilikuwa limesitishwa kutokana na vitendo vya kigaidi.

Ibada ya Misa takatifu ilianza kwa maandamano kutoka Parokia ya Burka, hadi kwenye Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi Olasti. Ibada hii imehudhuriwa na viongozi wa Kanisa, Serikali na vyama vya kisiasa, huku kukiwa na idadi kubwa ya Familia ya Mungu Jimbo kuu la Arusha.

Kardinali Pengo amewakumbusha waamini kwamba, Yesu Kristo ndiye mwanzilishi wa dini peke yake aliyeyamimina maisha yake kwa ajili ya kujenga Jumuiya ya Kikristo. Hata leo hii kuna watu bado wanaendelea kutoa maisha yao kwa ajili ya kutangaza Injili ya Kristo! Ifuatayo ni sehemu ya hotuba ya Kardinali Pengo pamoja na Viongozi mbali mbali wa Makanisa.


Ndugu zangu,

Nafasi hii inaunganisha mawazo ya furaha na uchungu kutokana na kilichotukutanisha leo. Mazingira haya yanaweka ugumu wa kupata cha kusema. Ila sisi ni watu wa imani. napenda kueleza imani yetu kama tunavyopaswa kuwa kwenye mazingira haya. Tumejumuika ili kuwaweka kwenye nyumba ya milele hawa marehemu, lakini pia tunatumia nafasi hii kubariki Kanisa.

Kila mbatizwa ni kiungo cha mwili wa Kanisa. Kila kiungo cha mwili kinapaswa kuungana na kichwa cha Mwili ambaye ni Yesu Mwenyewe. Kristo akipitia kwa mdomo wa mtume Paulo anatufundisha kuwa
"Msijaribu kushindana na uovu kwa uovu, lakini shindeni uovu kwa wema".

Katika viongozi waanzilishi wa dini, ni Yesu peke yake aliyetolea uhai wake kujenga imani ya wafuasi wake. Viongozi wengine hawajikutoa sadaka wenyewe, na baadhi wametoa sadaka ya maisha ya watu wengine kwa ajili ya kueneza imani yao. Sisi Wakristo Imani yetu inajengwa juu ya mwanzilishi wetu ambaye alitoa uhai wake ili kujenga imani yetu, na hakutoa uhai wa mtu yeyote kwa ajili ya kujenga imani yetu.

Katika masomo tuliyosikia leo, Somo la plili limetupa Neno la Mtume Paulo Rum:12:17 linasisitiza hilo: usishinde uovu kwa uovu, bali shinda uovu kwa wema.

Soma la Kwanza limeeleza kuwa Paulo na Sila wanateswa kwa ubaya mkubwa sana na kuwekwa gerezani kwa ubaya. Na baada ya kufunguliwa kwa muujiza, askari wa magereza alitaka kujiua, lakini Paulo na Sila wakatenda lililo jema kuokoa maisha yake. Ni baada ya wema huo wokovu ulifika kwa askari huyo na jamaa yake yote wakaweza kumwamini Mungu.


Nawauliza waumini: "Wale waliotekeleza ubaya huu, akija mbele yetu akasema ni mimi ndiye, tungefanya nini kama waumini kwa kufuata mfano wa Yesu?" Mimi nawaambia "Tujifunze kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo: 'Tusidiriki kulipia uovu kwa uovu, lakini tutende mema ili kushinda uovu'." Lakini haya hayaondoi majukumu ya serikali, ambayo yanabaki, na si mimi ninayepaswa kuyasema, wenye mamlaka wanayajua majukumu yao. Mimi nawaambia ninyi waumini.

Uovu si kitu kinachopendeza. Warumi waliwatesa wakristo kwa karne tatu, na haikusaidia chochote Himaya ya Warumi, ambayo baadaye ilisambaratika. Lakini imani yetu imebaki. Amemalizia kwa kusema: Tukio hili na tukio la mauaji ya Padre Mushi, isiwe sababu ya kuacha amani ya nchi yetu isambaratike. Lakini ni jukumu la wananchi wotte kuhakikisha nchi yetu haisambaratiki. Wenye mamlaka watimize wajibu wao. Sisi wakristo tusamehe, tusijibu uovu, tudumishe amani na upendo katika taifa letu.

Zifuatazo ni salama za rambi rambi kutoka kwa Askofu mkuu Dr. Alex Malasusa wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania.
Tumsifu Yesu Kristo.
Tunaagana na ndugu zetu katika mwili. Ni ibada yenye majonzi lakini ni yenye furaha kwa kuwa ndugu zetu wamelala katika imani na wataupata uzima wa milele. Natoa pole kwa wafiwa na kwa Baba Askofu Mkuu Josephat Lebulu. Yesu yu hai nasi tunaomwamini tutakuwa hai, hata miili itakapoharibika, tutaurithi uzima wa milele. Kama alivyosema Kardinali tusilipe ubaya kwa ubaya, lakini tusiwe waoga. Tumtangaze bila woga.
Tuelewe pia kuwa hatutahukumiwa tu kwa maovu tuliyotenda bali hata kwa mema ambayo hatukuyatenda Risasi wanazopigwa watumishi wa Mungu, mioto ya kuchoma makanisa, mabomu wanayotupiwa waumini, yasitukatishe tamaa. Askofu Malasusa anasema pia: Anatamani kama angefariki katika ibada kama marehemu hawa. Heri wafu wafao katika Bwana.
Naye, Askofu Mkuu Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha Kwa niaba ya mapade, watawa, walei wote alitoa pole kwa familia ya kanisa la Arusha. Kwa msiba huu anasema Wakristo tunajiuliza Mungu una ujumbe gani kwetu? Alitoa pole, kwa ndugu za marehemu watatu. Alitoa pole kwa wafiwa na kusema hakika tumeguswa sana na hata hatuna maneno ya kuelezea, tuliwatembelea mahospitalini na hakika watu wa Mungu wameumizwa sana. Pole sana kwa waumini wa kanisa hili na wakaazi wa eneo hili. Alisisitiza Tusikate tamaa!
Alitoa pole kwa wanafamilia ya Mungu wa Olasiti waliokuwa kwenye siku yao ya furaha ya kufungua parokia yao. Alitambua majitoleo waliyofanya wana Olasiti kwa kumjengea Mungu nyumba. Walijenga nyumba ya Mungu kwa nguvu zao bila ufadhili toka nje. Wakati wanataka kumtolea Mungu shukrani zao wamekatishwa, lakini hakuna kukata tamaa.
Alitoa shukrani kwa wale walioonesha moyo wa utu kulaani unyama ule. Aliishukuru serikali ya wilaya, mkoa na serikali kuu waliokuwa pamoja katika msiba huu. Na anamshukuru Waziri mkuu kwa uwepo. Anashukuru na Serikali ya Zanzibar kwa moyo wa utu, kwamba walimtembelea na waliwafariji wakristo wote wa Arusha. Aliwaambia waumini Msiogope! Kristo akiwa upande wetu hakuna atakayetushinda.
Kristo ametuambia katika Injili ya Yohane: Msifadhaike mioyoni mwenu, mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Yesu aliwaambia pia Msiogope. Mkijua mafundisho yangu, mtaujua ukweli na ukweli utawaweka huru. Anasema yeye kama Baba anawaambia, lazima ifikie mahali tuseme INATOSHA, Tumwambie Mungu IMETOSHA. Wenye nguvu na silaha watatushinda, lakini tukiwa na Mungu hatutashindwa. Paulo na Sila walisali Milango ya gereza ikafunguka. Tusali kwa nguvu zote. Alimaliza kwa kuwaaga marehemu akiwataja kwa majina na kumwambia kila mmoja kwa heri!








All the contents on this site are copyrighted ©.