2013-05-11 09:49:40

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania lataka Serikali isifumbie macho chokochoko za kidini!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania akitoa salam zake za rambi rambi kutonana na mauaji ya kinyama yaliyotokea kwenye Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi Olasiti, Jimbo kuu la Arusha hivi karibunina kupelekea watu watatu kupoteza maisha yao na wengine wengi kujeruhiwa anasema ni matokeo ya uhasama wa waamini wa dini mbali mbali nchini Tanzania, hali ambayo imekuwepo kwa takribani miongo mitatu sasa. Kadiri siku zinavyokwenda ndivyo uhusiano kati ya Wakristo na Waislam unavyozidi kuzorota na hivyo kusababisha wasi wasi mkubwa kwa wananchi kwa ujumla.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, damu ya mashahidi ni mbegu ya kustawisha Ukristo. Amewapatia pole wote walioguswa na msiba huu mkubwa na wenye kuhuzunisha. Ni tukio ambalo limesababisha maafa na hasara kubwa, lakini hata katika hali kama hii, Kanisa bado linaendelea kuhimiza umuhimu wa kuvumilia bila kutaka kulipiza kisasi.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, nchini Tanzania kumekuwepo na matukio kadhaa yanayoashiria hatima kama hii, tangu siku ile kundi la baadhi ya waamini wa dini ya Kiislam waliokutana kwenye Ukumbi wa Diamond Jubilee, tarehe 15 Januari 2011 kwa kutangaza na kudai kwamba, Tanzania inaongozwa na mfumo Kristo ambao umeenea nchi nzima na kwamba, Wakristo wamekuwa wakipendelewa na Serikali ya Tanzania katika mambo mengi. Kundi hili liliazimia kuukomesha Ukristo na kuufanya Uislam utawale nchini Tanzania.

Katika hitimisho la Makangomano yao hapo tarehe 16 Oktoba 2011 waliazimia kuua na kuuwawa. Jambo la kushangaza anasema Askofu Ngalalekumtwa Serikali ya Tanzania haikuchukua hatua makini licha ya kwamba Makongamano na Mihadhara hii inafanyika hadharani.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linavitaka vyombo vya ulinzi na usalama kutekeleza wajibu wake kwa weledi. Wagundue uovu na waovu washughulikiwe kisheria. Hii ndiyo njia muafaka ya kuirudisha Tanzania katika misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa. Katika hadha na madhulumu kama haya, Wakristo nchini Tanzania wanapaswa kuwa imara na thabiti katika imani yao na kamwe wasitetereke, kwani Maaskofu wanaendelea kuandamana nao katika hija ya imani na matumaini kama Familia ya Mungu inayowajibika.

Wakristo watambue kwamba, Kristo ndiye mchungaji wao, hata kama wakipita katika bonde la uvuli na mauti kamwe hawataogopa maana Yeye yuko pamoja nao na anawaongoza na kuwalinda.







All the contents on this site are copyrighted ©.