2013-05-10 13:52:17

Uwepo wa Papa katika mitandao ya kijamii unapania kuwafikia watu wengi zaidi, mahali waliko!


Ilikuwa ni tarehe 12 Desemba 2012, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita alipoanza kwa mara ya kwanza kutumia mitandao ya kijamii al maarufu kama twitter. Tangu wakati huo, idadi ya wafuasi wa Baba Mtakatifu katika mtandao wa twitter imeongezeka hadi kufikia zaidi ya millioni sita! Si haba kama kiatu cha raba!

Wakati wa mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, akaunti ya Papa ilisitishwa kwa muda na kuzinduliwa kwa nguvu kasi mpya na Baba Mtakatifu Francisko, jambo ambalo limepelekea kuongezeka kwa wafuasi wa Baba Mtakatifu Francisko katika akaunti yake.

Akaunti ya Papa inayojulikana kwa anuani ifuatayo: @Pontifex inasomeka kwa lugha ya Kiingereza, Kihispania, kiitaliani, Kireno, Kifaransa, Kijerumani, Kilatini, Kipoland na Kiarabu. Mara kwa mara Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican pia inakushirikisha ujumbe huu katika matangazo yake. Baba Mtakatifu Francisko amekuwa na mvuto wa pekee katika mitandao ya kijamii inayowashirikisha watu kutoka katika medani mbali mbali za maisha.

Baba Mtakatifu Francisko anatumia mitandao ya kijamii kwa lengo la kuinjilisha na kama njia ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari ilichangamotishe Kanisa kuwaendelea watu katika medani mbali mbali za maisha, kwani kuna umati mkubwa wa watu wenye kiu ya kutaka kusikia Habari Njema ikitangazwa maishani mwao!

Baba Mtakatifu Francisko katika siku za hivi karibuni ameongeza matumizi ya mitandao ya kijamii kiasi kwamba, walau kila siku anajitahidi kutuma ujumbe wa Neno la Mungu kwa mashabiki wanaomfuata kwenye akaunti yake ya twitter. Baba Mtakatifu anaendelea kuwahimiza vijana kutumia vyema karama na vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya mafao yao binafsi na mendeleo endelevu ya jamii inayowazunguka.

Anawataka vijana ambao kimsingi ndio watumiaji wakuu wa mitandao ya kijamii kuwa na ndoto ya mambo makubwa! Ni ujumbe wa maneno machache lakini unagusa uhalisia wa maisha ya mtu! Mama Kanisa anajiandaa kuadhimisha Siku ya Upashanaji Habari Duniani kwa Mwaka 2013, Jumapili tarehe 12 Mei 2013, sanjari na Siku kuu ya Kupaa Bwana Mbinguni.







All the contents on this site are copyrighted ©.