2013-05-09 08:01:12

Mitandao ya kijamii ni milango ya ukweli na imani, fursa mpya ya Uinjilishaji


Mama Kanisa daima ameendelea kusoma alama za nyakati katika dhamana na utume wake wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Kama ilivyokuwa kwa Mitume na Wafuasi wa Yesu wakati ule wa Kanisa la mwanzo, walijitosa kimasomaso bila kuogopa vikwazo na vipingamizi ambavyo wangeweza kukutana na vyo katika utekelezaji wa utume wao kwa watu wa mataifa.

Katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, Kanisa limejikuta linakabiliana na changamoto ya utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Huu ni ulimwengu mpya ambao unapaswa kumfahamu na kumtambua Mwenyezi Mungu, ili watu wengi waweze kufaidika na maendeleo haya ambayo kimsingi ni utajiri mkubwa wa binadamu.

Ni tafakari ya Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii anapoangalia jitihada za Mama Kanisa katika kumwilisha ujumbe wa Yesu Kristo katika mitandao ya kijamii, kama ambavyo anakazia Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika ujumbe wake kwa Siku ya 47 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni, itakayoadhimishwa hapo tarehe 12 Mei 2013. RealAudioMP3

Ni changamoto na mwaliko kwa Watoto wa Kanisa kuhakikisha kwamba, wanatambua na kuthamini mchango wa mitandao ya kijamii, ili kuweza kusaidia katika mchakato wa kumwilisha kweli za Kiinjili hata katika mitandao hii inayokuwa na kupanuka kwa kasi.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu katika Maadhimisho ya Siku ya 47 ya Upashanaji Habari Ulimwenguni unaongozwa na kauli mbiu “Mitandao ya Kijamii ni milango ya ukweli na imani, fursa mpya za Uinjilishaji”. Hii inaonesha dhamira ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika matumizi sahihi ya mitandao ya Kijamii kama milango ya ukweli na imani; haya ni majukwa mapya yanayoundwa na mitandao hii, ili kuweza kukutana na umati mkubwa wa vijana wa kizazi kipya ambao wana kiu na njaa ya kusikia Neno la Mungu, kuna haja kwa Mama Kanisa kuwafuata huko huko kwenye mitandao ya Kijamii, kama alivyofanya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita na mwendelezo huo tunauona kwa Papa Francisko kwa wakati huu.

Wachunguzi wa mitandao ya Kijamii wanabainisha kwamba, walau asilimia kubwa ya watumiaji wa mitandao wanashirikishana na kumegeana mambo yanayohusu Sinema na Muziki; idadi inayofuata ya wakazi hawa wanashirikishana maoni juu ya michezo na kiasi kidogo kabisa ni wale wanaojadili kuhusu masuala ya kidini. Mitandao ya kijamii ikitumiwa barabara na Mama Kanisa ni milango mingine mipya ya ukweli na imani.

Hapa ni mahali ambapo si tu kwamba, watu wanajipatia ufahamu, habari na burudani, lakini ni sehemu nyeti kabisa inayogusa undani wa mtu mzima: kiroho na kimwili. Umefika wakati kwa Kanisa kuhakikisha kwamba, mitandao ya kijamii inakuwa ni fursa makini kwa watumiaji kufahamu ukweli kuhusu Mungu na mwanadamu, ili kusaidia majiundo endelevu ya mwanadamu, kwa kusoma alama za nyakati na makini kwa mahitaji yake ya kiroho na kimwili, anasema Askofu mkuu Claudio Maria Celli.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alijitwalia dhamana ya kuhakikisha kwamba, anajitahidi kuwapo kwenye maskani ya watu, ili kuweza kuzima kiu na njaa ya watu hawa katika kumtafuta, kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Mwenyezi Mungu. Inaweza kuonekana kwamba, ni juhudi kidogo, lakini haya ni matone ya ukweli na upendo yanayomsindikiza mwanadamu katika hija yake ya maisha na mapambano yake katika jangwa la utupu na kinzani za maisha.

Idadi ya mashabiki wanaomfua Baba Mtakatifu kwa sasa imekwisha vuka watu millioni mbili na nusu, hii ina maana kwamba, ametambua njaa ya vijana wa kizazi kipya ambao ndio watumiaji wakubwa wa mitandao ya kijamii na sasa anaendelea kuwaonjesha ile hekima na upendo wa kibaba!

Askofu mkuu Claudio Maria Celli anasema, licha ya Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita na sasa Papa Francisko kujimwaga kwenye uwanja wa mitandao ya kijamii kwa heshima zote, lakini, hawakosekani wakorofi wanaotinga kwenye akaunti yake kwa matusi na maneno ya kejeli. Inasikitisha, lakini si jambo la kushangaza, kwani ni kielelezo cha kumong’onyoka kwa misingi ya maadili na utu wema.

Hata Yesu mwenyewe, licha ya kazi njema aliyotenda, watu wakamdhihaki, wakamcharaza kwa mijeledi, wakamtemea mate na hatimaye, wakamtundika Msalabani na hatimaye, kufa kifo cha aibu. Lakini baada ya Siku tatu, akafufuka kutoka katika wafu! Mshindi!

Baraza la Kipapa linabainisha kwamba, kuna ushuhuda mkubwa unaoendelea kujionesha miongoni mwa washabiki wanaomfuata Baba Mtakatifu, kwenye akaunti yake, huu ni mwelekeo chanya, ambao Baraza hili linapenda kuufuatilia kwa karibu zaidi, wakitambua kwamba, wote wanapenda na kuthaminiwa na Mwenyezi Mungu.

Wainjilishaji wanapaswa kusoma alama za nyakati na kutambua kwamba, wanatumwa kutangaza Injili ya Kristo kwanza kabisa kwa Jamii inayowazunguka sanjari na kutumia fursa mbali mbali zinazoendelea kuibuliwa na ulimwengu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari, kwa kupanua wigo na idadi ya walengwa katika huduma hii, lakini jambo la msingi ni majiundo makini kwa Wainjilishaji hawa! Ujumbe unaotangazwa unajikita kwa Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu! Huu ndio ujumbe unaopaswa kugusa mioyo, akili na maisha ya watu wa nyakati hizi.

Matumizi ya maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari ni changamoto iliyotolewa kwanza kabisa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, leo hii Vatican ni kati ya taasisi zenye mitandao mikubwa inayobeba inayotumiwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwa nia ya kuwasiliana pamoja na kulifahamu Kanisa. Kwa njia ya za mitandao ya kijamii, watu wengi wanapata fursa ya kufahamu ujumbe wa Baba Mtakatifu, vinginevyo wangeendelea kubaki katika giza.








All the contents on this site are copyrighted ©.