Makleri na watawa wanavyochakarika kutumia mitandao ya kijamii katika Uinjilishaji
mpya!
Jimbo kuu la Roma linajiandaa kikamilifu kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya 47 ya
Upashanaji Habari Ulimwenguni ambayo kwa mwaka huu, itaadhimishwa kwenye Siku kuu
ya Bwana Kupaa Mbinguni hapo tarehe 12 Mei 2013 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Mitandao
ya kijamii: milango ya ukweli na imani”.
Idara ya Mawasiliano ya Jimbo kuu
la Roma kwa kushirikiana na wadau mbali mbali katika sekta ya mawasiliano ya Jamii
inasema, hapo tarehe 9 Mei 2013 kutafanyika semina ya siku moja itakayokuwa ni fursa
kwa wadau wa sekta ya mawasiliano ya Jamii kutafakari kuhusu ujumbe wa Siku ya 47
ya Upashanaji Habari Ulimwenguni uliotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa
kumi na sita.
Washiriki watafahamishwa kuhusu tafiti zilizofanywa kuhusu Kanisa
na Mitandao ya Kijamii na kwa namna ya pekee jinsi ambavyo Makleri na Watawa katika
mchakato wa Uinjilishaji mpya wanavyochakarika kutumia mitandao ya Kijamii.
Mada
hii itawasilishwa na Professa Rita Marchetti kutoka Chuo Kikuu cha Perugia, Italia.
Ni utafiti ambao umefanywa kwa ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Milano
na Chuo Kikuu cha Perugia nchini Italia.