2013-05-07 09:11:42

Mchango wa maendeleo ya teknolojia ya habari katika dhamana ya Uinjilishaji mpya!


Njia za mawasiliano ya Jamii katika Nyakati za Uinjilishaji Mpya ndiyo mada itakayopembuliwa na wataalam wa mawasiliano ya Jamii katika Kongamano la Kitaifa lililoandaliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Canada. Kongamano hili litaanza kutimua vumbi hapo tarehe 8 na kuhitimishwa hapo tarehe 10 Mei 2013 Jijini Montreal. RealAudioMP3

Hii ni changamoto iliyotolewa na Mababa wa Sinodi ya Uinjilishaji Mpya iliyofanyika mjini Vatican mwezi Oktoba 2012 na sasa Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linapenda kutekeleza sehemu ya mapendekezo yaliyotolewa na Mababa wa Sinodi wakati huo. Wanasema, kuna uhusiano wa karibu sana kati ya dhamana ya Uinjilishaji na Njia ya za Mwasiliano ya Jamii.

Hii inatokana na ukweli kwamba, wafanyakazi katika vyombo vya upashanaji habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa wana mchango mkubwa katika dhamana na utume wa Uinjilishaji unaotekelezwa na Mama Kanisa sehemu mbali mbali za dunia hasa wakati huu ambapo kuna maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia ya habari. Wafanyakazi na vyombo vyao vya mawasiliano wanaweza kuwa ni mashahidi wakubwa wa imani Mama Kanisa anapojitahidi kuwaonjesha walimwengu uzuri na utamu wa Injili.

Kongamano la Mawasiliano Kitaifa nchini Canada, linapania pamoja na mambo mengine kuhakikisha kuwa linaweka mikakati madhubuti ambayo itasaidia kuweka msingi thabiti wa mwingiliano kati ya vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Mama Kanisa nchini Canada pamoja na vyombo vya habari vinavyomilikiwa na Sekta binafsi na Serikali ili kupanua wigo wa wasikilizaji, watazamaji na wasomaji wao.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linasema hii itakuwa ni nafasi nyingine tena kuangalia uwezekano wa kutumia mitandao ya Kijamii changamoto inayofanyiwa kazi kwa sasa na Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, kama njia nyingine zinazoweza kusaidia mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Kongamano hili linatarajiwa kufunguliwa na Askofu mkuu Paul-Andrè Durocher wa Jimbo kuu la Gatineau na atapembua kuhusu sauti mbili za Kanisa: ile inayojadili masuala ya Kimungu na sauti ya pili inapembua masuala yanayomgusa mwanadamu na vipaumbele vyake. Wajumbe wa Kongamano hili la kitaifa, wataangalia kwanza kabisa fursa, changamoto na vikwazo vinavyolikabili Kanisa katika azma ya Uinjilishaji Mpya.

Wawakilishi wa Baraza la Maaskofu Canada walioshiriki katika Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya, watachangia mawazo ya Mababa wa Sinodi katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Ni Kongamano litakalowashirikisha mabingwa na wataalam wa masuala ya mawasiliano ya Jamii ili kuweza kuzifanyia kazi changamoto za mawasiliano ya Jamii katika azma ya Uinjilishaji Mpya katika mikakati ya shughuli za kichungaji zinazofanywa na Kanisa Katoliki nchini Canada.








All the contents on this site are copyrighted ©.