Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amemwagiza Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa
Jamii, Dk. Seif Rashid awasiliane na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa (TAMISEMI) ili watafute njia ya kuinusuru Bohari ya Dawa (MSD).
Amesema
hawana budi kutafuta njia ya kuhakikisha kuwa asilimia 67 inayotengwa na Mfuko wa
Bima ya Afya (NHIF) kwa ajili ya kulipia dawa za wagonjwa mbalimbali inatumiwa ipasavyo
na si vinginevyo.
Ametoa kauli hiyo Jumapili, Mei 5, 2013 wakati akizindua
ghala jipya la kisasa la kuhifadhia dawa lililojengwa na Bohari ya Dawa, Kanda ya
Dodoma huko Kizota, nje kidogo ya mji wa Dodoma.
Ujenzi wa ghala hilo ambao
umegharimu sh. bilioni 9.9/-, umechangiwa na Serikali ya Marekani kupitia Shirika
lake la USAID na Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria
(Global Fund).
“Naibu Waziri kaeni na TAMISEMI ili itafute njia inayofaa kuzibana
Halmashauri zote ili fedha inayotolewa na Mfuko wa Bima ya Afya zote ziende kutumika
kwenye manunuzi ya dawa na si vinginevyo. Bima ya Afya wanataka asilimia 67 ya fedha
wanayotoa itumike kulipa dawa na asilimia 33 iwe kwa matumizi mengine,” alisema.
Alikuwa
kijibu risala ya MSD iliyosema Bohari ya Dawa inaidai Serikali kiasi cha sh. bilioni
52 ambazo zimelimbikizwa kutokana na madeni ya muda mrefu ya huduma za dawa, vifaa,
na vifaa tiba ambavyo taasisi hiyo ilitoa kwa vituoa vya afya vya Serikali pamoja
na hospitali zake.
Aliipongeza MSD kwamba licha ya mzigo mkubwa wa deni ilionao,
haijaacha Kutoa huduma ya kununua na kusambaza kwa wananchi. Alisema Serikali itajitahidi
kutafuta mbinu za kupunguza deni hilo katika bajeti ya mwaka huu.
Mapema, akimkaribisha
Waziri Mkuu kuzungumza na hadhara iliyohudhuria uzinduzi huo, Dk. Seif Rashid alisema
hivi sasa Bohari ya Dawa ilikuwa inakodisha mita za mraba 24,000 kwa ajili kupata
nafasi ya kuhifadhia dawa zinaingizwa kutoka nje ya nchi na kwamba kukamilika kwa
ujenzi wa ghala hilo, lenye mita za mraba 5,310 kutasadia kupunguza gharama hizo.
Naye
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa, Bw. Cosmas Mwaifwani alisema kuanzishwa kwa
taasisi kumesaidia kuongeza kiwango cha upatikanaji wa dawa kutoka asilimia 44 mwaka
1994 na kufikia asilimia 70 hadi 75 hivi sasa.
Alisema ili kuhakikisha dawa
zinapatikana kwa wakati hadi vijijini, Bohari ya Dawa imeshaingiza mikoa 10 kwenye
mfumo wake wa usambazaji wa dawa moja kwa moja hadi kwenye vituo vya afya badala ya
kuishia kwa Mganga Mkuu wa Wilaya.
Alisifu Halmashauri sita na hospitali moja
ya mkoa kwa kuwa mfano bora kwenye usimamizi na matumizi ya dawa zinazotolewa na kusambaza
na Bohari ya Dawa. Alizitaja Halmashauri hizo kuwa ni Iramba, Bariadi, Igunga, Chamwino,
Bahi na Sumbawanga. Aliitaja Hospitali ya Mkoa wa Iringa kuwa ndiyo iliyofanya vizuri
kuliko hospitali nyingine nchini.
Uzinduzi huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali
wa mkoa wa Dodoma, mwakilishi wa wahisani, wafanyakazi wa MSD na wakazi wa Kizota.