Mikakati ya Radio Maria katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya!
Radio Maria imeanza mkakati wa Uinjilishaji Mpya unaopania kwa namna ya pekee kuhakikisha
kwamba, Habari Njema ya Wokovu inawafikia watu wengi zaidi kwa njia za mawasiliano
ya kisasa pamoja na kuwahamasisha watu kufungulia Radio zinazoendeshwa na Majimbo
katika nchi zao, kama sehemu ya mchakato wa kuikaribisha sauti ya Kikristo kwenye
familia zao.
Radio Maria inajipanga kufungua ofisi kumi na moja, sehemu mbali
mbali za dunia kama sehemu ya mkakati wake wa kuwafikia wasikilizaji wengi zaidi.
Nchi ambazo ziko kwenye mpango huu ni pamoja na: India, Macao, Latvia na Haiti. Huku
kote ni mahali ambako kuna kiu ya imani, maadili na mwamko mpya wa maisha ya Kikristo
yanayojikita katika tunu msingi za Kiinjili: yaani: imani, matumaini,upendo na mshikamano
wa kidugu; daima wakiwa tayari kusimama kidete kutangaza Injili ya Uhai; Uvumilivu
na Majadiliano ya Kidini; Majiundo makini pamoja na Ushuhuda wa maisha.
Kuanzia
tarehe 8 hadi 10 Mei, 2013, kutafanyika Marathoni ya Radio Maria, kwa kuvishirikisha
vituo 60 ya Radio kutoka Afrika, Ulaya, Asia, Amerika na Oceania, kwa kuendesha vipindi
ambavyo vitajikita zaidi na zaidi katika maisha ya sala, ushuhuda pamoja na kushirikishana
mang'amuzi na vipaumbele vya maisha ya Kikristo katika ulimwengu wa utandawazi na
maendeleo ya sayansi na teknolojia kwa kutambua fursa na vikwazo ambavyo waamini wanaweza
kukumbana na vyo katika hija ya maisha yao ya kiimani, kiutu na kimaadili hapa duniani.
Hayo yamebainishwa na Padre Francisco Jose Palacios, Mratibu wa Radio Maria
World Family, kwenye Makao Makuu yake hapa mjini Vatican. Anasema, Radio Maria inapania
kujifunga kibwebwe ili kuhakikisha kwamba, inajikita zaidi katika Uinjilishaji kwa
njia ya Radio kwa kutangaza walau kwa masaa ishirini na manne, kama ilivyokuwa imebainishwa
kwenye mpango wake tangu awali. Dhamana hii inatekelezwa kwa njia ya sala pamoja na
majiundo makini ya maisha ya Kikristo na utu wema.
Kwa njia hii Radio Maria
itaendelea kutekeleza wajibu wake wa kimissionari kwa kuwaunganisha waamini na watu
wote wenye mapenzi mema katika nchi husika. Radio Maria inataka kuwashirikisha watu
uzuri wa imani wanaoiungama, adhimisha, ishi na kusali, kama sehemu ya mchakato wa
Uinjilishaji Mpya sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa
na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita; ushuhuda unaopewa kipaumbele
cha pekee na Papa Francisko wakati huu wa mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Hii ni imani katika matendo.
Itakumbukwa kwamba, Radio Maria Barani Afrika
ni mshirika mkuu wa Radio Vatican katika utekelezaji wa dhamana ya Uinjilishaji wa
Mpya. Tunamshukuru Mungu kwa ushirikiano huu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa
sehemu mbali mbali za dunia!