2013-05-03 07:54:48

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya sita ya Kipindi cha Pasaka


Tunaendelea na Tafakari ya Neno la Mungu, tayari tukiwa Dominika ya VI katika siku za furaha na nderemo, Mama Kanisa atuwekea Neno la furaha, Neno ambalo latufundisha kuwa Roho Mtakatifu ndiye mwalimu wa ukweli wote! RealAudioMP3

Katika somo la kwanza tunapata kuona Jumuiya ya kwanza ambayo ni mchanganyiko wa Wakristo waliotokea dini ya kiyahudi ambao wanasisitiza tohara na Wakristu waliokuwa wapagani ambao jambo hili kwao si la msingi. Kumbe kutokana na makundi haya mawili kuwa na mlengo tofauti kunakuwepo na matatizo ya hapa na pale.

Shida kubwa ambayo inashika kasi ni ile ambayo wapagani wanalazimishwa kuwa kwanza Wayahudi yaani kutahiriwa kwanza na ndipo waingie ukristu. Wapagani wanakataa hilo wakisema wokovu unatoka kwa Kristo na si toka mila za Kiyahudi. Mt Paulo anaona ni vema na sahihi kila mmoja kumfuasa Bwana akitokea kwenye utamaduni wake bila kulazimishwa kupitia utamaduni wa mwingine. Mt. Petro na Yakobo bado wanayo alama ya kiyahudi na hivi wamelala katika upande wa kutahilriwa kwanza kabla ya kuwa mkristo.

Mpendwa msikilizaji, shida hii itatatuliwa pamoja na shida nyingine kwa maongozi ya Roho Mtakatifu, yaani wataitisha Mtaguso wa Kwanza wa Yerusalemu. Basi, wanaamua kwa pamoja kuwa watafundisha Injili ya Bwana katika tamaduni zao, na kusisitiza kuwa mkristo hata hivyo ana haki ya kukataa mila fulani katika utamaduni wake, yaani kama kinapingana na Injili ya Bwana.

Kumbe, baada ya Mtaguso basi wokovu upo pasipo kutahiriwa cha msingi kumfuasa Kristo katika mapendo ya kweli. Kushika vema taratibu za ndoa takatifu, taratibu za kumtolea Mungu sadaka ambazo zinaambatana na mapendo kwa jirani na Mungu mwenyewe.

Katika somo la pili tunapata kuona faraja ambayo wataipata wale wote watakaoteseka kwa ajli ya Neno la Mungu na imani kwa ujumla. Mwishoni mwa nyakati uzima wa kimungu utakuwa ndani yao wote ambao wametoa jasholao kwa kumpenda Mungu. Mt Yohane yuko katika ndoto anaona mji wenye pande nne na milango3 kila upande, vikiwa ni alama ya uwezekano wa wokovu kwa wote (maana ya namba 4 katika Biblia-Nzima, wote) na milango yaashilia uwezekano wa kuingia katika uzima wa milele. Huko mbinguni hakutakuwa na litrujia wala mahekalu bali kumwona Mungu uso kwa uso. Tazama mpendwa furaha gani hiyo kuweza kumwona Mungu!

Ili tuweze kufikia mapendo na furaha ya mbinguni kadiri ya kitabu cha Ufunuo lazima tutekeleze yale ambayo Mwinjili anatuambia. Anasema mtu akinipenda mimi, akilishika Neno langu, mimi na Baba yangu tutakuja kwake. Kumbe, yatupasa kujenga umoja na Baba mapema hapa duniani. Na hakuna njia nyingine ya kwenda kwa Baba pasipo Kristo anayesma anionaye mimi amwona Baba. Yatupasa kuamini kina kazi za Kristo na mausia yake kwa ajili ya kufika kwa Baba. Neno la Mungu ni Kristo mwenyewew anayesema nasi kila siku kumbe tulipende tuliishi.

Mpendwa ona jinsi Kristo anavyotupenda kabla hajaondoka anahaidi Roho Mtakatifu ambaye atatufundisha yote, atakuwa mwalimu mfariji wetu. Hapa twaweza kuweka swali hivi Yesu hakufundisha yote? Alifundisha yote lakini mazingira yanabadilika na hivi tunahitaji msimamizi wa siku zote atakayeongoza historia mpaka mwisho wa nyakati. Mt. 28. Kristo anahaidi amani , si kama ile itolewayo na dunia kwa njia ya mabavu bali ijayo kama tunda la Pasaka, tunda la Roho mfariji, Roho wa amani.

Mpendwa, nikutakie furaha tele ya Pasaka ukijiandaa kwa ajili ya Sherehe ya kupaa Bwana Dominika ijayo. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.