2013-05-03 08:28:18

Sala ya Papa Francisko kwenye kaburi la Mtakatifu Francisko wa Assisi


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 2 Mei 2013 amesali kwenye kaburi la Mtakatifu Francisko wa Assisi kwa njia ya "webcam" na kumwomba Mtakatifu Francisko aweze kuiombea mioyo ya waamini ili iwe na amani.

Anawaomba Wafranciskani kusali kwa ajili ya maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro pamoja na kuwasaidia waamini na watu wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya mafao na ustawi wa Kanisa na Ulimwengu katika ujumla wake.

Baba Mtakatifu ameoneshwa pia toleo maalum la jarida linalochapishwa na Wafranciskani ambalo limetolewa kuonesha yale yaliyojiri wakati wa kuchaguliwa na hatimaye kuanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Baba Mtakatifu ameonesha utashi wa kutembelea mji wa Assisi, makao makuu ya Wafranciskani, mahali ambapo watu wengi wanakwenda kufanya hija ya imani, lakini zaidi kwa ajili ya kuombea amani kati ya watu na amani katika mioyo ya binadamu.

Akizungumzia kuhusu tukio hili la Baba Mtakatifu Francisko kusali moja kwa moja kwenye kaburi la Mtakatifu Francisko wa Assisi, Padre Enzo Fortunato anasema, hii inaonesha umuhimu wa njia mpya za mawasiliano ya kijamii zinavyoweza kutumika kama vyombo vya kusaidia kukuza na kuimarisha imani, lakini zaidi kama vyombo vya Uinjilishaji mpya, kama inavyojionesha kwa idadi kubwa ya sala zinazotumwa kwenye kaburi la Mtakatifu Francisko wa Assisi kutoka pande mbali mbali za dunia.

Tangu Baba Mtakatifu Francisko achaguliwe, watu wengi wamejielekeza zaidi katika sala ya matumaini na mshikamano katika hija ya imani wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha mwaka wa Imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.