2013-05-03 08:12:16

Karibu tena Papa mstaafu Benedikto XVI mjini Vatican!


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, Alhamisi, tarehe 2 Mei 2013 amerejea tena mjini Vatican baada ya kuishi kwenye Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo kwa takribani miezi miwili na kuelekea kwenye makazi yake mapya yaliyoko kwenye Monasteri ya Mater Ecclesiae mjini Vatican.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alipowasili kwenye uwanja wa ndege mjini Vatican amepokelewa na viongozi waandamizi kutoka Vatican wakiongozwa na Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali.

Msafara wa viongozi hawa ulipowasili kwenye lango la Monasteri ya Mater Ecclesiae umepokelewa na Papa Francisko kwa upendo, mshikamano na udugu. Viongozi hawa wawili walielekea kusali kwa pamoja kwenye Kikanisa kilichoko ndani ya Monasteri hii ambayo kwa sasa yatakuwa ni makazi ya Baba Mtakatifu Benedikto XVI katika hija yake maisha hapa duniani, akitumia muda wake mwingi kwa ajili ya kusali, kutafakari na kujisomea. Baba Mtakatifu mstaafu alisema mwenyewe kwamba, kwa sasa anapenda kuutumia muda wake kwa ajili ya kusali ili kuliombea Kanisa.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto katika makazi haya mapya ataendelea kuishi na Askofu mkuu Georg Gaenswein na Watawa waliokuwa wanatoa huduma wakati alipokuwa kwenye Makazi ya Kipapa mjini Vatican katika kipindi cha uongozi wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.