2013-05-03 10:29:06

Kanisa ni Jumuiya ya waamini inayopaswa kusimikwa katika upendo, mshikamano na udugu!


Kanisa halina budi kusikiliza kwa makini maongozi ya Roho Mtakatifu na kujitahidi kuyamwilisha katika maisha na utume wake kwa kuendelea kusoma alama za nyakati, huku wakitambua kwamba, Kanisa linatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, lakini, linapaswa kuwa imara na thabiti ili lisimezwe na malimwengu.

Ni Roho Mtakatifu ambaye amewawezesha Wakristo wa Kanisa la mwanzo kujifunga kibwebwe na kuanza kutoka katika miji yao, kifua mbele ili kumtangaza Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Roho Mtakatifu anahamasisha, anajenga na kuliimarisha Kanisa kutoka katika undani wake, huu ni mchakato endelevu unaojionesha hata leo hii katika maisha na utume wa Kanisa.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi, tarehe 2 Mei 2013 katika Ibada ya Misa Takatifu aliyoiadhimisha kwenye Kikanisa cha Domus Sancta Marthae kilichoko mjini Vatican na kuhudhuriwa na wafanyakazi kutoka katika Gazeti la L'Osservatore Romano linalomilikiwa na Vatican. Waamini wa Kanisa la mwanzo anasema Baba Mtakatifu walikabiliana matatizo na changamoto mbali mbali kutokana na kizani za mawazo na baadhi ya waamini kudhani kwamba, walikuwa wanaupendeleo wa pekee kabisa machoni pa mwezi Mungu kiasi hata cha kutaka kuwadharau na kuwabeza jirani zao.

Roho Mtakatifu akatekeleza wajibu wake: umoja, upendo, udugu na mshikamano ukapatikana miongoni mwa waamini kiasi cha kujiachilia kwa ajili ya kutangaza Injili ya Kristo, wakiwa wepesi kuchanja mbuga ili kuwashirikisha wale wasiomwamini Kristo ile furaha ya kuwa kweli mfuasi wa Kristo si tu kwa maneno bali kwa njia ya ushuhuda wa maisha.

Wakristo wanachangamotishwa na Kristo mwenyewe kujishikamanisha katika kifungo cha upendo ambacho ni kielelezo makini na utambulisho wa Fumbo la Utatu Mtakatifu. Jambo hili linawezekana ikiwa kama Wakristo watamwilisha ndani mwao na katika vipaumbele vyao Amri za Mungu ambazo kimsingi ni dira na mwongozo wa maisha adili. Waamini wajifunze kuishi katika upendo, daima wakitafuta toba na wongofu wa ndani, ili kuendelea kufaidi neema inayobubujika kutoka kwa Kristo kwa njia ya Roho Mtakatifu.

Waamini wajifunze pia kusamehe na kusahau; huku wakimwilisha huruma na upendo huu kwa njia ya matendo ya huruma hasa kwa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha. Hii inatokana na ukweli kwamba, waamini katika hija ya maisha yao hapa duniani wanakabiliana na dhambi pamoja na vishawishi kadha wa kadha.

Waamini watambue ubinadamu wao na wawe wepesi kukimbilia huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya Sakramenti za Kanisa. Kanisa liendelee kufungua malango ya matumaini kwa wote wanaotaka kuonja upendo wa Mungu!







All the contents on this site are copyrighted ©.