Waamini wanamsubiri Papa Francisko kusali Rozari pamoja naye, Jumamosi tarehe 4 Mei
2013
Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 4 Mei 2013, Saa 12:00 jioni, anatarajiwa
kusali Rozari takatifu na waamini watakaokuwa wamekusanyika katika Kanisa kuu la Bikira
Maria mkuu lililoko mjini Roma. Itakumbukwa kwamba, hii ni mara ya pili kwa Baba Mtakatifu
Francisko kwenda Kanisa hapo tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa kama Khalifa wa
Mtakatifu Petro.
Lakini wakati huu, anakwenda rasmi kama sehemu ya utekelezaji
wa mzunguko wa hija kwa Makanisa makuu yaliyoko mjini Roma. Mara atakapofika Kanisani
hapo atapewa Msalaba na kuubusu baadaye atakwenda kutoa heshima kwa Sanamu ya Bikira
Maria Afya watu wa Roma "Salus Popoli Romani" kama inavyojulikana kwenye viunga vya
Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu.
Ibada ya Rozari Takatifu ambayo kimsingi
ni muhtasari wa Injili itaendeshwa kwa lugha ya Kiitalia, wakiongozwa na Baba Mtakatifu
Francisko. Jumamosi ijayo, Kanisa litatafakari Matendo ya Utukufu.
Akihojiwa
na Gazeti la L'Oservatore Romano linalotolewa na Vatican kila siku, Padre Fernàndes
Rodriguez, mkuu wa Mapadre wauungamishaji wanaotoa huduma yao kwenye Kanisa kuu la
Bikira Maria Mkuu mjini Roma anasema kwamba, kwa sasa wako Wadominikani kumi na wawili
wanaotekeleza wajibu na utume wao chini ya uongozi wa Baraza la Toba ya Kitume.
Ni
utume unaohitaji hekima ya maisha ya kiroho, kwa kuwaheshimu na kuwajali wale wanaokimbilia
huruma na upendo wa Mungu katika Sakramenti ya Upatanisho ili kuwasaidia kuonja upendo
huu kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Jumuiya hii ya Mapadre Wadomenikani bado wanayo
kumbu kumbu hai asubuhi na mapema, tarehe 14 Machi 2013 Papa Francisko alipofika kwenye
Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu kutolea heshima yake kwa Mama wa Mungu na Kanisa,
akaacha shada la maua kwenye Sanamu ya Bikira Maria.
Uwepo wake tena ni mwaliko
kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kusali na kumwombea katika
maisha na utume wake; ili aweze kuwa na afya ya roho na mwili pamoja na kuendelea
kuwaimaarisha ndugu zake katika imani, matumaini, mapendo na umoja kamili.
Baba
Mtakatifu Francisko alipotembelea kwa mara ya kwanza katika Kanisa kuu la Bikira Maria
Mkuu, aliwataka waungamishaji kuwa na huruma na mapendo. Padre ambaye anatumia muda
wake mwingi kwa ajili ya kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa, inakuwa kweli ni zawadi kubwa
ambayo Mwenyezi Mungu anawakirimia watu wake. Sakramenti ya Upatanisho inawahitaji
Mapadre watakatifu, wanaotambua dhamana na wito ambao wamekabidhiwa na Mama Kanisa.
Utume huu unapaswa kutekelezwa katika hali ya sala na ukimya. Mapadre pia
watambua umuhimu wa kujipatanisha na Mungu kabla ya kuwapatanisha wengine, ili pia
waweze kuonja huruma na upendo unobubujika kutoka katika Sakramenti ya Upatanisho.