Siku kuu ya Vesakh: pendeni, lindeni na kudumisha uhai wa binadamu
Wakristo na Wabudha wanahamasishwa kupenda, kulinda na kudumisha uhai wa binadamu,
ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe kutoka kwa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya
Kidini kwa waamini wa dini ya Kibudha wanaposherehekea Siku kuu ya Vesakh kwa mwaka
2013. Huu ni mwendelezo wa mchakato unaopania kwa namna ya pekee kudumisha uhusiano
wa kidini na kirafiki na waamini wa dini ya Kibudha.
Baba Mtakatifu Francisko
alipokuwa anaanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, alikazia umuhimu wa
majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali duniani, kwa kutambua kwamba,
Kanisa lina dhamana kwa ulimwengu katika harakati za kupenda, kulinda na kuendeleza
kazi ya uumbaji ambayo mwanadamu amekabidhiwa na Mwenyezi Mungu.
Lengo ni
kuwasaidia: maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; wanaoteseka na kudhulumiwa
ili waweze kupata haki, amani pamoja na kudumisha upatanisho.
Ili amani iweze
kupatikana na kushamiri miongoni mwa watu wa mataifa kuna haja kwanza kabisa kuheshimu,
kuthamini na kulinda zawadi ya uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa
mama yake. Hivi ndivyo alivyokuwa ameandika Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi
na sita, katika ujumbe wake wa kuombea amani duniani kwa mwaka 2013.
Kardinali
Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini katika ujumbe
huu anabainisha kwamba, Kanisa Katoliki linaheshimu na kuthamini Mapokeo ya Dini ya
Kibudha hasa katika kuheshimu uhai wa binadamu, taamuli, ukimya na ukawaida unaojionesha
katika uhalisia wa maisha. Majadiliano ya pamoja baina ya waamini wa dini hizi mbili
yanaonesha kwa namna ya pekee jinsi ambavyo wanaheshimu zawadi ya uhai.
Hii
ni changamoto ya kuondokana na utamaduni wa kifo, kwa kukazia: maadili, utu wema,
upendo kwa jirani pamoja na Amri za Mungu. Kanisa Katoliki linathamini na kuenzi yale
ambayo ni kweli na matakatifu yanayopatikana kwenye dini nyingine. Kutokana na changamoto
iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa, Wakristo na Wabudha wakishirikishana amana
za Mapokeo yao ya kidini wanapaswa kujenga na kudumisha mazingira ya kupenda amani,
kulinda na kutetea uhai wa mwanadamu.
Hii inatokana na ukweli kwamba, maisha
ya binadamu ni jambo takatifu, lakini limeendelea kukabiliana na kinzani kutoka kwa
watu binafsi na Jamii za watu, changamoto kwa waamini wa dini hizi mbili kusimama
kidete kupinga mambo yote yanayohatarisha uhai wa binadamu, kwa kuamsha tena dhamiri
na maadili mema ndani ya Jamii ili watu kweli waweze kupenda, kulinda na kuenzi uhai
wa mwanadamu katika hatua zake zote.
Kardinali Jean Louis Tauran anahitimisha
ujumbe katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Vesakh kwa kuwataka Wabudha kuendelea kushirikiana
kwa kuguswa na mahangaiko ya Familia ya binadamu kwa kuenzi utakatifu wa maisha ya
mwanadamu. Na kwa maneno haya, anawatakia waamini hao amani na furaha wanapoadhimisha
Siku kuu ya Vesakh.