2013-05-02 07:47:45

Sakramenti ya Ubatizo ni mlango wa Imani kwa Kristo na Kanisa lake!


Nyumba inaweza kuwa nzuri utakavyo lakini bila mlango ni bure. Gari na vyombo vyote vya usafiri vinaweza kuwa vya muhimu sana lakini bila milango havifai kitu. Mlango ni chombo kinachokuingiza katika mahusiano na vitu vingine. RealAudioMP3
Ndani ya pipa letu vijana leo hewani tunachomoka na maana ya Porta Fidei, Mlango wa Imani. Seat bado zipo, karibu ndani, chukua nafasi, funga mkanda vizuri tuanze kupaa ndani ya studio za Radio Vatican.
Ubatizo ni Sakramenti, ishara wazi ya neema isiyoonekana. Ubatizo unatuondolea dhambi ya asali pamoja na adhabu zake, unatufanya kuwa watoto wa Mungu na Kanisa. Kumbe kijana unatakaswa kwa Sakramenti hii, na unaingia katika mahusiano kati yako na Kanisa na kati yako na Mungu. Mlango huu ukishaupita hakuna kurudi nyuma. Hata ukianza kutapatapa mara uende huku mara kule mara ukashifu dini na kadhalika, wewe unabaki mkristo, sababu umebatizwa. Ukiwa ndani ya mahusiano na Mungu unapaswa kujitahidi kutunza vema mahusiano hayo.
Fungua moyo na akili yako ili kumpokea Kristo na kudumu naye. Safari yako ya mahusiano, safari ya muungano kati ya Mungu inaanza na Ubatizo na inadumu milele iwapo utaishi kwa uaminifu siku zote. Mahusiano hayo unayoanza hapa duniani yanaendelea katika uzima wa milele.
Bila shaka unajiuliza, unahitaji nini katika mlango huu na muunganiko wako na Mungu. Katika Kanisa la Mungu unapobatizwa, unabatizwa kwa kuzingatia Imani uliyo nayo kwa Mungu. Bila Imani ubatizo huo hauna nguvu, sababu ubatizo ni mlango unaokuingiza katika safari ya Imani na mahusiano ya kudumu na Mungu. Kumbe unaalikwa kuikiri imani sio tu unapobatizwa, bali kila siku ya maisha yako. Imani hiyo uikiri kwa moyo radhi.
Imani hiyo haiishii kuikiri kanisani tu, au kwa maneno tu. Imani hiyo uikiri kila wakati na kila mahali unapojikuta. Uwe kazini, shuleni, sokoni, sehemu ya biashara, nyumbani, safarini na kadhalika. Ikiri Imani yako kwa matendo pia. Mtume Yakobo anatufundisha: yafaa nini imani yako iwapo unaikiri kwa maneno tu lakini hauishuhudii kwa matendo. Kumbe matendo yako ni ya msingi sana. Onesha wazi kwa matendo ya kuwa wewe ni mkristu unaishi maadili ya kikristu bila aibu bila woga. Tena jisikie fahari juu ya imani yako, ukiweza kuzingatia hilo utakuwa mtu wa furaha sana.
Baada ya kuingia katika muungano na Mungu kwa Sakramenti ya Ubatizo, unadumu katika mahusiano hayo kwa Sakramenti zingine. Kila Sakramenti ni ishara wazi ya neema ya Mungu isiyoonekana. Huwezi kupokea kwa halali Sakramenti yeyote bila kuwa umebatizwa.
Mwenyezi Mungu amejishusha na kuamua kuwa na mahusiano na muungano nawe kwa njia mbali mbali na katika nyakati tofauti. Hii yote ni sababu anakupenda. Kumpokea kwako katika Sakramenti ya Ubatizo, mlango wa imani. Kudumu kwako ndani yake kunaongozwa na Upendo. Upendo ulio nao kwake Mungu ni upendo huo huo uwe nao kwa wengine bila ubaguzi.
Ukisema unampenda Mungu bila kuwapenda wengine utakuwa muongo. Na ukisema unatenda mema kwa wengine bila kuishi maadili ya kikristu na kumwamini Mungu pia utakuwa muongo. Mkiri na kumwamini Mungu kwa upendo wa kweli, kwa moyo radhi na akili timamu.
Mlango wa moyo wangu umefunguliwa na Kristu ili kumpenda Mungu na kuwapenda watu wote. Nakualika wewe pia ufungue mlango wa moyo wako na udumu katika hilo. Ndivyo ninanvyosepa kutoka Studio za Radio Vatican, sauti ya kinabii Padre Celestine Nyanda.








All the contents on this site are copyrighted ©.