Umuhimu wa kazi na Tafakari kuhusu Fumbo la maisha ya Yesu Kristo!
Baba Mtakatifu Francisko katika katekesi yake, Jumatano tarehe Mosi Mei, 2013 ameitolea
kwa heshima ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi pamoja na Bikira Maria Mama wa Yesu ambaye
Mwezi Mei, Kanisa linafanya Ibada maalum kwa ajili yake changamoto ya kumtafakari
Yesu Kristo katika hija ya maisha ya kila siku.
Baba Mtakatifu anabainisha
kwamba, Mtakatifu Yosefu ambaye kitaaluma alikuwani Seremala, ni mtu anayewakumbusha
waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema dhamana na umuhimu wa kazi. Anasema,
kazi ni sehemu ya mpango wa Mungu kwa ulimwengu, mwaliko wa kuitekeleza kwa juhudi,
maarifa na kuwajibika zaidi kwa ajili ya mafao ya kazi ya uumbaji na utu wa mwanadamu
aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, ukosefu
wa fursa za ajira ni tatizo na changamoto inayopaswa kufanyiwa kazi kwa kuzingatia
mshikamano wa kijamii pamoja na sera makini. Anawataka vijana kuendelea kutafuta fursa
za ajira kwa matumaini bila ya kukata tamaa, kwa kuwekeza zaidi katika elimu, kazi
na mahusiano bora na wengine.
Mtakatifu Yosefu ni mfano wa mtu aliye sali
katika ukimya, akawa karibu zaidi na Yesu, changamoto ya kuangalia ni kiasi gani cha
muda ambao waamini wanatenga kwa ajili ya kusali na kulitafakari Neno la Mungu. Mwezi
Mei ni mwezi wa Rozari Takatifu unaowapatia waamini nafasi ya kutafakari Fumbo la
Maisha ya Kristo. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Bikira Maria na Mtakatifu
Yosefu ili waweze kuwasaidia kuwa waaminifu katika utekelezaji wa majukumu ya kazi
zao za kila siku pamoja na kuinua akili na mioyo yao kwa Yesu katika sala.
Baba
Mtakatifu Francisko ametambua uwepo wa: waamini, mahujaji na wageni wanaozungumza
lugha ya Kiingereza, wote hawa amewatakia kheri, baraka na amani ya kutoka kwa Kristo
Mfufuka. Anawaalika waamini kusali kama Familia pamoja na Familia kwani familia inayosali
pamoja hiyo itadumu na kuimarika. Anawataka vijana kujikita zaidi katika masomo, kazi,
matendo ya upendo pamoja na kujenga urafiki wenye tija!
Kwa waamini na mahujaji
wanaozungumza lugha ya Kiarabu, Baba Mtakatifu anawataka kuwa na ujasiri katika utekelezaji
wa majukumu yao kwa njia ya sadaka, daima wakiwa na matumaini hai bila kukata tamaa.
Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko amesema, Mei Mosi ya Mwaka huu,
Kanisa linafanya kumbu kumbu ya miaka miwili tangu Papa Yohane Paulo wa pili alipotangazwa
kuwa Mwenyeheri, changamoto kwa kila mwamini kuhakikisha kwamba, maisha yake yanafumbatwa
katika imani, upendo na ujasiri wa kitume kama ule uliooneshwa na Mwenyeheri Yohane
Paulo wa pili.
Baba Mtakatifu ametambua pia uwepo wa Mapadre kutoka Chuo Kikuu
cha Kipapa cha Mtakatifu Paulo, Roma; Watawa wa mashirika mbali mbali wanaoadhimisha
mikutano yao mikuu hapa Roma, waamini kutoka Parokia mbali mbali na vyama vya kitume,
kila mmoja anachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa mwaminifu kwa wito wake kwa njia
ya ushuhuda makini.
Vijana wajitahidi kumpenda na kumfuasa Kristo kwa uaminifu;
wagonjwa watolee shida na mahangaiko yao katika Fumbo la Upendo wa Yesu aliyemwaga
Damu yake Azizi; wanandoa wapya wawe waaminifu katika maagano yao na waoneshe upendo
wa Kristo kwa Kanisa lake.
Mara baada ya katekesi, Baba Mtakatifu Francisko
ametumia muda mrefu kwa ajili ya kusalimia na kuzungumza na waamini na mahujaji waliokuwa
kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro. Baadhi ya watu wameshangazwa walipomwona
Baba Mtakatifu akibadilishana Kikofia cha Kipapa na Padre, akakivaa hapo hapo bila
hata ya kufikiri mara mbili! Matendo makuu ya Mungu kwa watu wake!