2013-05-01 10:07:32

Siku kuu ya Wafanyakazi ijenge na kudumisha haki jamii!


Baraza la Maaskofu Katoliki India linayataka Mashirika yanayongozwa na kusimamiwa na Kanisa kuhakikisha kwamba, yanatoa kipaumbele cha kwanza katika kulinda na kusimamia haki jamii; kwa kutoa mishahara inayozingatia haki pamoja na kudumisha haki msingi za wanawake hasa wahamiaji.

Maaskofu Katoliki India katika ujumbe wao katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Wafanyakazi Duniani Mwaka 2013 wanakazia kwamba, Kanisa katoliki katika Mafundisho Jamii linatambua na kuthamini mchango wa vyama vya wafanyakazi kama kielelezo cha mshikamano wa kijamii.

Majimbo na Parokia mbali mbali zimetakiwa kuanzisha dawati litakalojadili pamoja na mambo mengine huduma za kichungaji kwa wafanyakazi wahamiaji ili kuweza kukidhi mahitaji yao: kiroho pamoja na kuweza kuingizwa katika maisha ya jamii inayowazunguka.

Ni jukumu lao kuhakikisha kuwa wanawasaidia wafanyakazi wanaoishi katika hali duni kwa njia ya vyama vya wafanyakazi ili viweze kuwaletea nafuu na maisha bora zaidi. Hifadhi ya jamii ni jambo ambalo kwa sasa linapewa msukumo wa pekee na Baraza la Maaskofu Katoliki India. Maaskofu wanasema katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Wafanyakazi Duniani kwa mwaka huu wananchi wanapaswa pia kujielekeza katika mapambano dhidi ya ajira za watoto pamoja na kuwapatia wafanyakazi mishahara mzuri.







All the contents on this site are copyrighted ©.