Kuweni na ari pamoja na moyo mkuu, tayari kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya
Kristo na Kanisa lake! Lakini angalieni...!
Kardinali Mauro Piacenza, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Makleri, hivi karibuni
amehitimisha hija ya kichungaji nchini Poland, kwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu
iliyohudhuriwa na umati mkubwa wa Majandokasisi na Wanovisi kutoka sehemu mbali mbali
za Poland, wakionesha ile furaha ya kutaka kumfuasa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka
kutoka katika wafu. Ni vijana wenye ari na moyo mkuu ambao wako tayari kujitoa kwa
furaha kwa ajili ya kumtumikia Mungu na jirani zao kwa njia maisha na wakfu na utume
wa Kipadre.
Katika mahubiri
yake, Kardinali Piacenza amewaonya vijana hawa kukumbuka kwamba, ile ndiyo yao kwa
Kristo na Kanisa lake halina budi kububujika kutoka katika undani wa maisha yao na
wala si kwa kujisikia tu! Hili ni jibu linalogusa undani wa mtu wa kujitoa bila ya
kujibakiza, hali ambayo inampatia mtu utambulisho wa kuwa kama Kristo Mchungaji mwema.
Mapadre na watawa hawataweza kupata furaha ya kweli ikiwa kama wito wao hawataweza
kuzamisha jibu lao katika uhalisia wa maisha kwa kushikamana na Kristo.
Vijana
wanatakiwa kila wakati kufanya tafakari ya kina ili kuweza kung’amua sababu na lengo
na miito yao ndani ya Kanisa kama kweli inaendana na mpango wa Kristo katika maisha
yao ili waweze kufanya uamuzi wa busara badala ya kujutia maisha baadaye!
Kardinali
Piacenza anawaambia vijana kwamba, ikiwa kama hawawezi kujitoa bila ya kujibakiza
kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake katika maisha ya Upadre na Utawa, wawe na ujasiri
wa kusema, hapa kwa hakika maji ni mazito na hivyo kuamua kurudi nyumbani kuendelea
na maisha mengine yatakayompendeza Mungu na binadamu. Kristo anapaswa kuwa ni kielelezo
cha majitoleo ya hali ya juu yanayoonesha utimilifu wake kwa njia ya mateso, kifo
na ufufuko wake, kwa maneno mengine majitoleo ya Kristo yanajionesha katika Msalaba.
Huu ni mwaliko wa kufanya tafakari ya kina kuhusu maana ya wito wa kipadre
na kitawa; dhamana na wajibu wake kwa Kristo na Kanisa lake na kama kweli wako tayari
kufanya hija ya Njia ya Msalaba pamoja na Kristo hadi Mlimani Kalvari, ili kuyamimina
maisha yao kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu; ili kuadhimisha na kugawa Mafumbo
ya Kanisa kwa watu wa Mungu.
Vijana watambue kwamba, mbele yao baada ya Upadrisho
watapewa taji la miiba; mikono na miguu yao itafungwa kwa misumari. Mikono yao iliyotobolewa
itaadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu na kuwaondolewa watu dhambi zao. Miguu yao
mizito itakayokuwa inachuruzika damu, itapaswa kuwapeleka sehemu mbali mbali za dunia
ili kutangaza Injili ya Kristo.
Kardinali Piacenza anabainisha kwamba, Yesu
aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu ni kielelezo makini cha ukuhani na
ufuasi unaopaswa kutekelezwa na watoto wa Kanisa kwa njia ya sadaka na majitoleo makubwa.
Ni mwaliko wa kujifunza kumwilisha fadhila za Kikristo katika maisha ya kila siku
kwa kutambua kwamba: ufukara, useja na utii ni nadhiri ambazo zinapaswa kutolewa ushuhuda
na Mapadre pamoja na Watawa katika ulimwengu mamboleo. Majandokasisi na Wanovisi wakati
wa majiundo yao watambue na kukuza fadhila hizi zitakazokuwa ni: dira, nguzo na kielelezo
cha maisha na utume wao kwa sasa na kwa siku za usoni.
Leo wao wanajiona kuwa
ni Waseminari na Wanovisi, lakini kesho watapadrishwa na kuweka nadhiri zao kuwa ni
Mapadre na Watawa. Watambulikane kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao, kama ambavyo
alivyowahi kukazia Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.
Watambulikane
katika Fumbo la Mwili wa Kristo yaani Kanisa; waonekane pia katika Maadhimisho ya
Fumbo la Ekaristi Takatifu, tayari kujimega na kujitoa kwa ajili ya Kristo na Kanisa
lake.
Kardinali Mauro Piacenza, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Makleri
anasema, miaka ya malezi na majiundo ya Kipadre na Kitawa itumike vyema kwa ajili
ya majiundo ya: kiakili, kiroho na kichungaji kwani mbele yao kuna changamoto nyingi
zinazoendelea kuibuliwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na
teknolojia.
Watambue na kujenga uhusiano na mshikamano wa dhati na Kristo
na kwamba, Upadre na Utawa wao ni kwa ajili ya huduma kwa Mungu na Jirani. Watafute
muda wa kufanya tafakari ya kina pamoja na kumwomba Bikira Maria ili aweze kuwasaidia
na kuwaongoza katika wito wao wa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na
Kanisa lake.