Pokeeni zawadi ya Roho Mtakatifu ili kumtolea Kristo ushuhuda kwa njia ya maisha!
Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu ambamo
ametoa Sakramenti ya Kipaimara kwa Wakristo kutoka pande mbali mbali za dunia, kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, Jumapili tarehe 28 Aprili 2013, aliwaweka
waamini walioimarishwa kwa Mapaji ya Roho Mtakatifu chini ya ulinzi na maombezi ya
Bikira Maria wakati wa sala ya Malkia wa Mbingu.
Baba Mtakatifu anawaalika
waamini hao kujifunza kutoka kwa Bikira Maria maana ya kuishi ndani ya Roho Mtakatifu
sanjari na kuukaribisha upya wa maisha unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Bikira
Maria alitunga mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, changamoto kwa kila Mkristo kukaribisha
Neno la Mungu pamoja na kumkaribisha Yesu katika maisha yake, huku akijitahidi kumpeleka
kwa wengine.
Bikira Maria alikuwepo wakati wa Roho Mtakatifu alipowashukia
Mitume walipokuwa kwenye chumba cha juu. Baba Mtakatifu anasema, kila wakati waamini
wanapokusanyika kwa ajili ya kusali wanategemezwa kwa uwepo wa Roho Mtakatifu na Bikira
Maria, Mama wa Kristo, ili kuweza kupokea zawadi ya Roho Mtakatifu, hatimaye, kuweza
kumtolea ushuhuda Yesu Mfufuka.
Baba Mtakatifu Francisko ameyasema haya kwa
namna ya pekee akiwaelekea zaidi wale ambao wameimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara
kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Anawataka wamwombe Bikira Maria
ili awasaidie kuwa wasikivu kwa kile ambacho Bwana anataka kutoka kwao, daima wakijitahidi
kuishi kadiri ya matakwa ya Roho Mtakatifu.
Baba Mtakatifu alitambua uwepo
wa waamini kutoka sehemu mbali mbali za dunia waliofika katika Maadhimisho ya Mwaka
wa Imani. Amewakumbuka na kuwaombea wakristo wote watakaopokea Sakramenti ya Kipaimara
wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.
Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu
Francisko ameyaelekeza mawazo na sala zake kwa watu waliofikwa na maafa ya kuangukiwa
jengo la kiwanda cha kutengeneza nguo huko Dakar, Bangaladesh. Ameonesha mshikamano
wake wa upendo kwa njia ya sala na familia pamoja na wote walioguswa na msiba huu
mkubwa. Anaomba kutoka katika undani wa moyo wake, wahusika wote kuhakikisha kwamba,
wanasimama kidete kulinda utu na usalama wa wafanyakazi.
Mara baada ya Maadhimisho
ya Misa takatifu na Sala ya Malkia wa mbingu, Baba Mtakatifu Francisko alizunguka
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kusalimiana na waamini waliokuwa wamefurika
na kujaza viunga vya Vatican, kila mmoja akiwa na hamu ya kutaka kusalimiana naye.
Baba Mtakatifu ametumia muda mrefu kidogo baada ya Misa Takatifu kusalimiana
na kuzungumza na Mapadre walioshiriki katika Ibada ya Misa Takatifu kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, hii inaonesha moyo wa upendo na mshikamano wakidugu
unaopaswa kujionesha miongoni mwa Mapadre wanapotekeleza wajibu wao kwa Kristo na
Kanisa lake.