2013-04-29 09:02:05

Pokeeni mapaji ya Roho Mtakatifu ili muweze kubadilika na kuimarishwa wakati wa majaribu na magumu ya maisha; mkishikamana na Kristo!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili ya tano ya Kipindi cha Pasaka, tarehe 28 Aprili 2013 ametoa Sakramenti ya Kipaimara kwa Wakristo 44 kutoka sehemu mbali mbali za dunia, katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, na kuhudhuriwa na bahari ya watu!

Katika mahubiri yake, Baba Mtakatifu anasema, mbele ya Mungu mambo yote ni mapya kwani yanabadilika na kuonesha: wema, uzuri na ukweli. Mwenyezi Mungu kwa njia ya Roho Mtakatifu anamwendea na kumletea mwanadamu mabadiliko ya ndani changamoto ya kutambua kwamba, mwanadamu yuko katika hija ya kuiendea Yerusalemu mpya, siku ambayo watabahatika kuonana na Yesu Kristo uso kwa uso na kuishi pamoja naye milele yote katika upendo.

Baba Mtakatifu anawaambia waamini kwamba, mambo mapya kutoka kwa Mwenyezi Mungu ni tofauti kabisa na yale yanayotolewa na walimwengu kwani mapya ya dunia ni mambo ya mpito! Roho Mtakatifu anapowaletea waamini mabadiliko ya ndani anawataka kufanya pia mabadiliko katika ulimwengu wanamoishi, mwaliko kwa kila mwamini kumfungulia Roho Mtakatifu mlango wa maisha yake, ili aweze kuongozwa naye na kuendelea kupokea msaada kutoka kwa Mwenyezi Mungu unaowafanya kuwa wapya kutokana na uvuvio wa upendo wa Mungu unaotolewa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuchunguza dhamiri zao kila siku jioni ili kuangalia ni kwa jinsi gani wameweza kumwilisha ndani mwao upendo wa Mungu kwa marafiki, ndugu na jamaa au kwa wazee na wale wanaohitaji zaidi. Wakifanikiwa kutekeleza haya kwa hakika watagundua kwamba, inapendeza.

Hija ya maisha ya Kanisa na waamini katika ujumla wake si rahisi kwani daima imesheheni vikwazo na majaribu. Kumfuasa Kristo ni kuruhusu Roho wake aweze kugeuza ile sura ya giza na matendo yasiyompendeza Mungu; kuwaondolea dhambi pamoja na kuwakinga kutokana na vikwazo vinavyowazunguka na vile ambavyo viko ndani mwa mioyo yao!

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, matatizo na majaribu ya maisha ni njia inayompeleka mwamini katika utukufu wa Mungu, kama ilivyokuwa kwa Yesu Kristo aliyetukuzwa na Baba yake wa mbinguni kwa njia ya Msalaba. Vikwazo na majaribu ni sehemu ya hija ya maisha ya mwamini hapa duniani, jambo ambalo kamwe lisiwafanye waamini kukata tamaa kwani wanayo ndani mwao ile nguvu ya Roho Mtakatifu inayowawezesha kuyashinda yote haya!

Baba Mtakatifu kwa namna ya pekee, amewaalika Wakristo walioimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara kuwa imara katika hija ya imani na matumaini kwa Yesu Kristo kwani hii ndiyo siri ya mafanikio katika hija ya maisha ya waamini! Anawatia moyo pale wanapokumbana na mawimbi mazito ya bahari, kiasi kwamba, wasifuate mkumbo katika maisha, kwani hili ni jambo jema kwa ajili yao.

Wawe na ujasiri wa kukabiliana na mawimbi mazito katika maisha yao ya kila siku, kwani Yesu mwenyewe anawakirimia ujasiri huu, ikiwa kama wataambatana na kuendelea kuungana na Mwenyezi Mungu kwani wao ni kama matawi, ikiwa kama wataimarisha urafiki na Mungu kwa kumpatia nafasi katika maisha yao.

Baba Mtakatifu anasema, hili ni jambo muhimu sana kukumbuka hasa pale wanapojisikia kuwa maskini, wanyonge na wa dhambi kwani Mwenyezi Mungu daima anawaimarisha pale wanapohisi kwamba, ni wanyonge, anawatajirisha kutokana na umaskini wao; anawapatia toba, wongofu wa ndani na msamaha wa dhambi. Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma, yuko tayari kuwasamehe watoto wake wanapomkimbilia wakiomba msamaha, jambo la msingi, ni kujiaminisha katika kazi ya Mungu.

Waamini wakiambatana na Mungu, kwa hakika wanaweza kufanya mambo makubwa, kwani atawakirimia furaha ya kuwa ni wafuasi na mashahidi wake amini. Baba Mtakatifu anahitimisha mahubiri yake kwa kuwataka Waamini, lakini kwa namna ya pekee kabisa, wale ambao wameimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara kuwa na ndoto ya mambo makubwa, kwani wamechaguliwa na Kristo kwa ajili ya mambo makubwa zaidi. Mambo mapya kutoka kwa Mwenyezi Mungu, majaribu ya maisha pamoja na kuwa imara katika Kristo ni mambo msingi katika maisha ya mwamini.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumfungulia Mungu malango ya maisha yao, ili waweze kupokea mapaji ya Roho Mtakatifu yanayopania kuwabadilisha na kuwaimarisha wakati wa majaribu pamoja na kuendelea kuwaimarisha na kushikamana na Bwana, kwani hii ndiyo furaha ya kweli!







All the contents on this site are copyrighted ©.