2013-04-25 09:42:32

UN: tekelezeni wajibu wenu ili kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria


Viongozi wa Jumuiya ya Kimatafa kunako mwaka 2000 walijiwekea Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015; mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria na Ukimwi ni kati ya malengo hayo.

Kuna baadhi ya nchi ambazo zimeonesha mafanikio makubwa katika kupambana na ugonjwa wa Malaria kwa kuboresha huduma za afya, uchunguzi wa magonjwa, matumizi ya vyandarua vvyenye dawa sanjari na matumizi ya dawa sahihi ni kati ya mambo ambayo yamesaidia kupunguza vifo vya mamillioni ya wagonjwa wa Malaria duniani.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika ujumbe wake kwa Siku ya Malaria Duniani kwa Mwaka 2013 anabainisha kwamba, licha ya jitihada zote hizi lakini, Malaria bado ni ugonjwa unaoendelea kusababisha vifo vya watu wengi duniani; na kwa namna ya pekee Barani Afrika.

Hii inatokana na ukweli kwamba, hakuna taarifa rasmi za ugonjwa wa Malaria; kuna baadhi ya maeneo ambayo wadudu wa Malaria wamekuwa sugu pamoja na matumizi hafifu ya vyandarua. Haya ni mambo ambayo yanakwamisha juhudi za mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria. Licha ya wadau kuchangia katika Mfuko wa Mapambano dhidi ya Ugonjwa wa malaria, lakini bado kuna pungufu ya dolla za kimarekani billioni 3.

Kuna nchi kumi ambazo ugonjwa wa Malaria umeendelea kuwa sugu na chanzo kikuu cha vifo vya watu wake. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anabainisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inawajibu wa kuchangia mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria katika nchi hizi ili kuokoa maisha ya watu. Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na mapambano dhidi ya Ukimwi na Kifua Kikuu duniani. Kampeni ya maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani kwa Mwaka 2013 ni wekeza katika siku za usoni. Shinda Malaria.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kwamba, mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria yanapania si tu katika kuboresha afya ya watu, bali ni sehemu ya mchakato wa kujenga jamii ya kimataifa yenye afya bora, changamoto kwa viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kutekeleza ahadi zao katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria, kwani huu ni ugonjwa ambao watu wanaweza kujikinga wasiugue!







All the contents on this site are copyrighted ©.