2013-04-25 09:12:57

"Huyo ni mimi ... tangu kutungwa mimba tumboni mwa mama yangu"


Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania lilizindua kampeni ya zawadi ya maisha kwa mwaka 2013, inayoongozwa na kauli mbiu "Huyo ni mimi... tangu kutungwa mimba tumboni mwa mama yangu" inayopania kuwahamasisha waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Kampeni hii inawajumuisha watu mbali mbali ambao kwa hiyari yao wenyewe wameamua kutoa picha za watoto, ndugu na jamaa katika umri mbali mbali ili kuonesha ukuaji wa mtu, tangu pale anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti inapomfika. Watu wanaelezea umuhimu wa maisha dhidi ya utamaduni wa kifo unaoendelea kushika kasi sehemu mbali mbali za dunia.

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linabainisha kwamba, Kanisa linapenda kusherehekea zawadi ya maisha, tangu pale mtoto anapotungwa mimba, kwani maisha ni sehemu ya haki msingi za binadamu. Wazazi wana wajibu wa kwanza kabisa wa kulinda watoto ambao bado wangali tumboni mwa mama zao dhidi ya vitisho na sera za utoaji mimba. Kwa kuthamini Injili ya Uhai, watu wataweza kuwa na ujasiri wa kutetea maisha ya watu wengine sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.