2013-04-24 10:31:19

Msilegeze kamba Malaria bado inapukutisha maisha ya watu Barani Afrika


Jumuiya ya Kimataifa inapoadhimisha Siku ya Malaria Duniani kwa Mwaka 2013, Bara la Afrika linapaswa kushiriki kikamilifu kwa kutambua kwamba, bado kuna asilimia 33% ya vifo Barani Afrika vinavyosababishwa na ugonjwa wa Malaria, kadiri ya taarifa ya Malaria Duniani kwa Mwaka 2012.

Mikakati ya mapambano dhidi ya Malaria imepelekea kuokoa maisha ya watu millioni 1.1. Bado kuna idadi kubwa ya watoto wanaopoteza maisha yao kutokana na Malaria Barani Afrika, jambo ambalo haliwezi kuvumiliwa kamwe.

Dr. Luis Sambo, Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani, Kanda ya Afrika anabainisha kwamba, kauli mbiu ya maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani kwa Mwaka 2013: Wekeza katika siku za usoni. Shinda Malaria inakwenda sanjari na utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015.

Huu ni mwaliko kwa wadau mbali mbali kuchangia kwa hali na mali katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria Duniani pamoja na kuwa na sera makini dhidi ya Malaria bila kusahau kujenga na kuimarisha ushirikiano wa dhati. Utamaduni wa usafi wa mazingira, matumizi sahihi ya vyandarua na dawa pamoja na kuendeleza tafiti zitakazosaidia kufutilia mbali ugonjwa wa Malaria ni kati ya mambo msingi yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mapambano dhidi ya Malaria Duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.