2013-04-24 07:16:37

Imani hai inajidhihirisha katika matumaini na mapendo


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa rasmi na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inaendelea kukushirikisha barua ya kichungaji kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Maaskofu wanasema, Imani hai inajidhihirisha katika matumaini na mapendo. Wanajadili pia changamoto mbali mbali ambazo Wakatoliki Tanzania wanakumbana nazo. Kutujuza zaidi ndani ya viunga vya Radio Vatican ni Sr. Gisela Upendo Msuya. RealAudioMP3

Imani ya kweli inajidhihirisha katika matumaini na upendo. Fadhila hizi tatu za kimungu haziachani (Rej. 1Kor 13:13). Upendo, kama anavyoandika Mt. Agostino, kwa kawaida unatanguliwa na imani: “Upendo kwa Mungu na kwa jirani utatoka wapi bila imani? Anawezaje mtu kumpenda Mungu asiyemwamini?” Imani ni ufunguo unaotuingiza katika mji wa Mungu, mji ambao wale wanaoishi ndani yake, wanatembea kwa miguu ya matumaini na upendo. Imani ya kweli ni lazima ijidhihirishe kwa kukua katika matendo ya upendo (Rej. Yak 2:14-18 ).

Huu ni ushuhuda wa upendo, unaojenga imani na kuikuza imani. “Imani inakua pale inapotiwa katika maisha kama uzoefu wa upendo uliopokelewa na pale inaposhirikishwa kwa wengine kama uzoefu wa neema na furaha. Inatufanya kuzaa matunda, kwa sababu inapanua ndani ya mioyo yetu matumaini na kutuwezesha kuwa na ushuhuda ulio hai: hakika, inafungua mioyo na akili za wale wanaosikiliza kuuitikia mwaliko wa Bwana wa kushikilia neno lake wa kuwa wafuasi wake.” Imani pia inajenga matumaini na matumaini ni dhihirisho la kile tunachokiamini. Kwa hiyo Mwaka wa Imani ni mwaliko pia wa kukua katika fadhila hizi za kimungu.

Changamoto mbali mbali hasa za mahusiano na watu wa Jumuiya nyingine za Kikristo na dini nyingine.

Kama Wakristo Wakatoliki wa Tanzania tunaiishi imani yetu tukiwa katika jamii iliyo pia na watu wenye imani tofauti na imani yetu. Kati ya hawa wapo wanaoamini baadhi ya yale tunayoamini na wengine ambao hawaamini kabisa kile tunachokiamini. Pamoja na tofauti zetu za kiimani, Kanisa Katoliki linaamini katika uhuru wa kuabudu na linaheshimu watu wa dini na madhehebu yote. Kwa kuzingatia ukweli huo, Kanisa limejitahidi sana kuunda mazingira ya mazungumzano kati yake na wakristo wa madhehebu mengine na watu wa dini nyingine kwa lengo la kukuza mshikamano, kuheshimiana na kuelekeza nguvu zetu katika kudumisha utu wa binadamu na amani ya Taifa letu.

Katika siku za karibuni yamejitokeza matukio yasiyopendeza na ya kusikitisha. Kashfa dhidi ya dini na madhehebu mengine zinazidi kuendelea na hali hiyo inaanza kuonekana kuwa ni utamaduni usio rasmi wa Taifa letu kwa sababu unafumbiwa macho.
Yamekuwepo matukio ya kuchomwa moto kwa nyumba za ibada na baadhi ya vyombo vya habari vinavyomilikiwa na madhehebu ya dini kutumika kuanzisha na kuendeleza malumbano, uchochezi, chokochoko na kashfa za kidini. Hali hii haijengi na ni kukosa heshima kwa imani za wengine. Kanisa linaamini kwa dhati kabisa kuwa, “Katika matumizi ya uhuru wowote, watu lazima waheshimu kanuni ya kimaadili ya uwajibikaji wa binafsi na wa kijamii.”
Kama Kanisa Katoliki nchini tunawaomba waamini wetu msishawishike kutenda jambo lolote kinyume na maelekezo ya upendo wa kiinjili. Kuweni macho mkidumu katika sala. Kuweni wapole kama hua, lakini wenye busara kama nyoka (rej. Mt 10:16). Tunaomba msitumie muda wenu kuhubiri juu ya imani zisizowahusu. Jikiteni katika kuijua na kuiishi imani yetu kwa kina.
Lakini pia tunaziomba mamlaka kuu kutoruhusu kujengeka utamaduni wa kusia mbegu za chuki na migongano inayoteteresha imani. Tusikubali kufika mahali ambapo matukio yasiyo ya kawaida yakaonekana kuwa ni ya kawaida, hasa yanapoendelea kutokea na nguvu za dola zikaonekana kuwa kimya au kuzidiwa nguvu.








All the contents on this site are copyrighted ©.