2013-04-23 08:28:49

Jumuiya ya Kimataifa yasikitishwa na mauaji ya watu 187 nchini Nigeria


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon amesikitishwa na taarifa ya vifo vya watu 187 vilivyotokea nchini Nigeria, baada ya mapambano makali kati ya Jeshi la Serikali na Kikundi cha Boko Haram yaliyotokea mwishoni mwa Juma, huko Kaskazini Mashariki mwa Nigeria.

Katibu mkuu anasema hakuna sababu yoyote ile ya kimsingi inayoweza kuhalalisha mauaji ya watu hawa. Kila upande unaohusika unawajibika kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu pamoja na kulinda maisha ya raia.

Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama nchini humo kufanya uchunguzi wa kina kuhusiana na mauaji ya raia. Anaendelea kusubiri taarifa ya Tume aliyounda ili kuangalia uwezekano wa kutoa msamaha kwa wana mgambo wa Boko Haram ambao wamekuwa ni tishio kwa usalama na maisha ya wananchi wa Nigeria. Taarifa zinaonesha kwamba, Boko Haram hawana mpango wa kufanya mazungumzo na Serikali ya Nigeria.







All the contents on this site are copyrighted ©.