2013-04-19 11:48:54

Msamaha unaweza kutolewa kwa Kikundi cha Boko Haram ikiwa kama watatubu pamoja na kulipa fidia waathirika wa vitendo vya kigaidi walivyotenda!


Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria ameunda Tume ya watu ishirini na sita, ili kuanzisha mchakato wa majadiliano kati ya Serikali na Kikundi cha Boko Haram, ili kuweza kufikia muafaka wa amani na utulivu, Kaskazini mwa Nigeria, sehemu ambayo kwa miezi kadhaa imekuwa ni uwanja wa mashambulizi na mauaji ya kujitoa mhanga.

Tume hii imepewa jukumu la kutafuta mbinu zitakazotumiwa na Serikali ili kutoa msamaha kwa wahusika wa Kikundi cha Boko Haram, sanjari na kusalimisha silaha katika kipindi cha siku 60. Tume pia itatoa mapendekezo ya jinsi gani waathirika wa vitendo haramu vilivyofanywa na Kikundi cha Boko Haram watakavyosaidiwa.

Tume hii inaongozwa na Waziri asiyekuwa na Wizara maalum Bwana Kabiru Tanimu Turaki na kuwajumuisha wajumbe kutoka katika dini, wabunge, wanajeshi, wasomi, wanasheria, wanadiplomasia na watetezi wa haki msingi za binadamu.

Takwimu zinaonesha kwamba, katika kipindi cha Mwaka 2009 zaidi ya watu 1,500 waliuwawa kikatili na Kikundi cha Boko Haram, ambacho kilijielekeza katika kuyashambulia Makanisa na Waamini waliokuwa Makanisani. Hivi karibuni, Kamanda mkuu wa Kikundi hiki Bwana Abubakar Shekau alikanusha jitihada za kutaka kuwapatia msamaha. Bado mashambulizi na madhulumu ya kidini yanaendelea nchini Nigeria watu wasiokuwa na hatia wanauwawa kinyama na makazi yao kuchomwa moto.

Kardinali John Olorunfemi Onaiyekan, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nigeria anabainisha kwamba, kutoa msamaha kwa Kikundi cha Boko Haram inawezekana kuwa ni moja ya njia ya kusimamisha mashambulizi dhidi ya watu wasiokuwa na hatia.

Katika vita, kuna wakati inawabidi wahusika wakuu kukaa chini kitako na kuanza kujadili uwezekano wa kupata ufumbuzi wa mgogoro wao, bila shaka hiki ni kipindi maalum cha kujadiliana na Boko Haram, kwani ni vyema zaidi kufanya majadiliano kuliko kuachilia mtutu wa bunduki kuendelea kurindima na hivyo kufyeka maisha ya watu wasiokuwa na hatia.

Kardinali Onaiyekan anasikitika kusema kwamba, kutoa msamaha kwa Kikundi cha Boko Haram bila wao wenyewe kutambua makosa waliyowatendea wananchi wa Nigeria kwa kusababisha mauaji makubwa na uharibifu wa mali ni sawa na kumpigia mbuzi gitaa! Kikundi cha Boko Haram kinapaswa kutubu na kukiri makosa yao; wawajibishwe kulipa fidia kwa waathirika wa vitendo vya kigaidi walivyoendesha. Masharti haya mawili yakitekelezwa, msamaha unaweza kutolewa na haki kutendeka, kwani haki na msamaha ni chanda na pete.







All the contents on this site are copyrighted ©.