2013-04-18 08:31:10

Huduma kwa maskini na wanyonge itolewe kwa moyo wa ukarimu na unyenyekevu!


Padre Germini Longio Lukoka kutoka Jimbo Katoliki la Same, Tanzania ni kati ya waamini, mahujaji na watalii waliokuwepo kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumatano tarehe 17 Aprili 2013 wakati wa Katekesi ya Baba Mtakatifu Francisko. RealAudioMP3

Padre Lukoka katika mahojiano na Radio Vatican anasema, kwamba, Baba Mtakatifu Francisko katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro anaendelea kutoa changamoto kubwa kwa Waamini kuhudumia katika hali ya unyenyekevu kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kama alivyofanya Kristo mwenyewe katika Fumbo la Umwilisho linalopata utimilifu wake katika Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo.

Anasema, tangu Baba Mtakatifu Francisko achaguliwe kuliongoza Kanisa Katoliki, Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro umekuwa ukifurika kwa umati mkubwa wa waamini, mahujaji na watalii. Ameonesha upendo wa pekee kwa wanyonge, akina mama na watoto.

Hii ni changamoto kwanza kabisa ya kuwalinda na kuwathamini watoto kwa kuwapatia malezi bora: kiroho na kimwili ili waweze kukua na kukomaa katika hekima na kimo. Wanawake wawezeshwe kikamilifu ili waweze kutekeleza utume na dhamana yao katika maisha ya Kijamii na Kikanisa.

Padre Longio anahitimisha mahojiano haya na Radio Vatican akimtakia kheri na fanaka Baba Mtakatifu Francisko anapojiandaa pia kusherehekea Siku ya Mtakatifu Joji, Shahidi, somo wake hapo tarehe 23 Aprili 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.