Jumuiya ya Kimataifa inalaani vitendo vya kigaidi mjini Boston, USA
Kardinali Seàn O'Malley, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Boston, Marekani, anaungana na
viongozi pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuwakumbuka na kuwaombea wale wote
walioathirika kutokana na mlipuko wa bomu uliotokea wakati wa mbio za marathoni mjini
Boston, Jumatatu, tarehe 15 Aprili 2013 na hivyo kupelekea watu watatu kupoteza maisha
yao na wengine 141 kulazwa Hospitalini kutokana na majeraha waliyopata.
Anatoa
salam za rambi rambi kwa wale waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki zao katika mlipuko
huo pamoja na kuendelea kuwaombea wote waliopata majeraha ili waweze kupona haraka.
Kardinali
Seàn anawashukuru wote waliojitoa kuokoa maisha ya wanariadha wa Marathoni na kwamba,
iwe ni changamoto ya kuhakikisha kuwa na kuna ulinzi na usalama wa kutosha kwa watu
na mali zao. Anasema, Kanisa litashirikiana na wadau wengine ili kuonesha mshikamano
wa upendo kwa wote walioathirika kutokana na maafa haya na kwamba, wote kwa pamoja
wapanie kuanza mchakato wa uponyaji wa madonda haya.
Viongozi mbali mbali
wa Jumuiya ya Kimataifa wanalaani vitendo hivi vya kigaidi dhidi ya watu wasiokuwa
na hatia.