2013-04-16 07:29:10

Juhudi za Makanisa Zimbabwe katika mchakato wa kudumisha misingi ya haki na amani kuelekea kwenye uchaguzi mkuu


Wananchi wa Zimbabwe wameanza maandalizi kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka huu, baada ya kupitisha Katiba kwa kura ya maoni na hivyo kufanya mabadiliko makubwa yanayopania pamoja na mambo mengine, kupunguza madaraka makubwa aliyokuwa nayo Rais, kusimamia haki msingi za binadamu pamoja na kudumisha misingi ya haki na amani. RealAudioMP3

Kwa kuzingatia historia ya Zimbabwe kwa miaka ya hivi karibuni, iliyopelekea machafuko ya kisiasa na hatimaye kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Baraza la Makanisa Zimbabwe limeunda Tume ya Kiekumene ya Wasimamizi wa Uchaguzi mkuu, yenye dhamana ya kukoleza moyo wa majadiliano, ili kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Tume hii inatekeleza wajibu wake kabla, wakati na baada ya uchaguzi mkuu na inasimamiwa na Tenda Maregere. Haya ni malengo ambayo Baraza la Makanisa Zimbabwe lilijiwekea kwa kitambo kidogo, kwa sasa yanafanyiwa utekelezaji wake, kadiri ya taarifa iliyotolewa na Shirika la Habari la Misna.

Makanisa nchini Zimbabwe yamekuwa yakichangia kwa kiasi kikubwa katika kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na umoja wa kitaifa, bila kusahau upatanisho pale ambapo kinzani na migogoro ya kisiasa ilipojitokeza; mambo ambayo yamekuwa ni sehemu ya historia ya wananchi wa Zimbabwe tangu wakati wa harakati za kupigania uhuru kutoka katika utawala wa Mwingereza.

Tume ya Mabaraza ya Makanisa pamoja na mambo mengine inapania kukuza moyo wa majadiliano miongoni mwa wananchi wa Zimbabwe, kudhibiti mchakato mzima wa upigaji kura ili haki, uhuru na ukweli viweze kutawala na hatimaye, Zimbabwe iweze kuwapata viongozi watakaochaguliwa kwa kura halali wakitambua dhamana na wajibu wao katika kuiendeleza nchi yao. Tume itakuwa na wajibu wa kusema haraka iwezekanavyo pale ambapo kutakuwepo na ukiukwaji wa haki msingi za binadamu.

Vyama vikuu vya upinzani vinavyotoana jasho kwa sasa ni ZANU-PF kinachoongozwa na Rais Robert Mugabe pamoja na Chama cha Democratic Movement for Change kinachoongozwa na Waziri mkuu wa Zimbabwe Bwana Morgan Tsvangirai; wapinzani wakuu waliopelekea machafuko ya kisiasa nchini Zimbabwe kunako mwaka 2008.








All the contents on this site are copyrighted ©.