2013-04-15 12:03:59

Watu wanaanza kupoteza matumaini ya maisha kutokana na vita nchini Afrika ya Kati


Baraza la Maaskofu Katoliki Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati linasema, hadi sasa wanakabiliana na hali ngumu ya maisha, kiasi cha kuwakatisha watu wengi tamaa ya maisha kutokana na machafuko ya kisiasa yanayoendelea nchini mwao. Wanajeshi wa vikosi vya waasi wanaendelea kupora mali za watu hali ambayo inaendelea kuwajengea watu hofu na mashaka.

Waasi hawa wanaorodha ya majina ya watu wanaotaka kuwashughulikia katika operesheni maalum. Maaskofu wanaiomba Jumuiya ya Kimataifa kusaidia juhudi za kuleta haki, amani, upatanisho na mshikamano wa kweli nchini humo. Maaskofu wanabainisha kwamba, kwa takribani miaka ishirini, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati wameendelea kushuhudia machafuko ya kisiasa yaliyopelekea watu wengi kupoteza maisha na mali zao pamoja na kukwamisha juhudi za wananchi kujikomboa kutoka katika umaskini, ujinga na maradhi, kwani amani ni jina jipya la maendeleo endelevu ya watu.

Vita haina macho wala pazia; imepelekea nchi yao kuwa ni kati ya nchi maskini zaidi duniani, ingawa rasilimali wanazo, lakini kwa bahati mbaya rasilimali hii ambayo ingeweza kutumika katika mapambano dhidi ya ujinga, umaskini na maradhi maadui wakuu wa kitaifa, sasa inatumika kwa ajili ya mauaji, nyanyaso na dhuluma za kijinsia kwa wananchi wasiokuwa na hatia.

Shirika la Kipapa linalotoa misaada kwa Makanisa Hitaji, katika taarifa yake linaonesha kwamba, kuanzia mwaka 2002 hadi sasa kuna jumla ya miradi 240 iliyogharimiwa na Shirika hili kwa ajili ya maendeleo endelevu ya wananchi katika Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati.

Kiasi cha Euro millioni mbili zimetumika kwa ajili kuwajengea uwezo Makleri, kugharimia shughuli za kichungaji, ujenzi wa Makanisa na nyumba za kitawa pamoja na kuwasomesha viongozi wa Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.