Katika maadhimisho ya kumbu kumbu ya mwezi mmoja tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa
kuliongoza Kanisa, Jumamosi, tarehe 13 Aprili 2013 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu
iliyohudhuriwa na Wanajeshi wa Kikosi cha Zimamoto cha Vatican na Watawa wa Upendo
kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae martha, kilichoko mjini Vatican.
Papa amewakumbusha
kwamba, hata katika mahangaiko, mateso na shida mbali mbali anazoweza kukabiliana
nazo mwamini, kamwe asithubutu kutafuta njia ya mkato bali wajiaminishe kwa Mwenyezi
Mungu. Waamini wa Kanisa la Mwanzo, kadiri ya Matendo ya Mitume, walijikuta wanaanza
kulalamikiana na kubaguana katika huduma mambo ambayo yalikuwa yanadhohofisha umoja
na mshikamano wa upendo miongoni mwa wafuasi wa Kristo. Mitume wakachukua uamuzi wa
kuwakutanisha na kujadiliana kwa pamoja na hatimaye, wakapata suluhisho la matatizo
yao.
Mitume walibainisha kwamba, dhamana yao ya kwanza ni kusali na kutangaza
Habari Njema ya Wokovu; kumbe Mashemasi saba walioteuliwa walipewa dhamana ya kutoa
huduma ya upendo ambayo ni mwendelezo wa huduma na mshikamano wa upendo unaofanywa
na Mama Kanisa sehemu mbali mbali za dunia. Kristo yuko daima pamoja na wafuasi wake
na kamwe hawezi kuwaacha wakaangamia.
Baba Mtakatifu anasema, hivi ndivyo ilivyotokea
pale mitume wake walipokuwa wameelemewa na hofu pamoja na woga, akawatokea na kuwaambia
wasiogope. Hata kama waamini wanakosea, wasikate tamaa, bali watambue kwamba, Yesu
yuko pamoja nao. Wachunguze pale walipokosea, wajiwekee mikakati ya kusahihisha na
kurekebisha pamoja na kujipa moyo wa kusonga mbele kwa imani na matumaini zaidi. Waamini
kamwe wasitafute njia ya mkato katika maisha!