2013-04-13 08:55:38

Maaskofu wa IMBISA wataka uchaguzi huru na wa haki nchini Zimbabwe


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, IMBISA, limezitaka nchi wanachama wa Jumuiya ya Uchumi na Maendeleo Kusini mwa Afrika, SADC, kuhakikisha kwamba, uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika nchini Zimbabwe kwa mwaka huu, unakuwa huru na wa haki. Ombi la IMBISA limewakilishwa hivi karibuni kwa Rais Emilio Guebuza, Rais wa Msumbiji na Mwenyekiti wa SADC kwa sasa.

Wawakilishi wa IMBISA wanaiomba SADC ambayo imekuwa mstari wa mbele katika kukoleza majadiliano ya kisiasa na hatimaye kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kuhakikisha kwamba, amani na utulivu vinarejeshwa: kabla, wakati na mara baada ya uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe ili kuepuka kinzani na migogoro ya kijamii iliyoibuka kunako mwaka 2008 na hivyo kusababisha hali ngumu ya maisha kwa wananchi wa Zimbabwe.

Ili haki, amani, utulivu, ukweli na uwazi viweze kutawala wakati wa mchakato mzima wa uchaguzi mkuu, wajumbe wa IMBISA wanasema kuna haja kwa vyama vya kisiasa nchini Zimbabwe hasa vile vyenye ushawishi mkubwa kuwa na makubaliano watakayotekeleza wakati wa uchaguzi mkuu na kwamba, wasimamizi wa uchaguzi kimataifa waruhusiwe kuangalia mwendo mzima wa uchaguzi miezi mitatu kabla. Wanaweza pia kubaki nchini Zimbabwe walau kwa mwezi mmoja baada ya uchaguzi, ili kuwa na uhakika wa mchakato mzima wa uchaguzi. Mara nyingi vurugu na kinzani zimekuwa zikijitokeza mara baada ya kutangaza matokeo.

Rais Emilio Guebuza amewashukuru wajumbe wa IMBISA na kwamba, majadiliano haya yamefanyika katika hali ya maelewano ya hali ya juu na amewashukuru wajumbe wa IMBISA kwa kuguswa na hali ya wananchi wa Zimbabwe wakati huu wanapojiandaa kwa uchaguzi mkuu. Maaskofu wa IMBISA wamewahakikishia wakuu wa Nchi za SADC uwepo na mchango wao katika kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu Kusini mwa Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.