2013-04-11 10:44:05

Watu wanaohudumiwa na Caritas Italia wanamshukuru na kumpongeza Papa Francisko


Baba Mtakatifu Francisko amewaandikia watu wanaohudumiwa kwenye vituo vya huduma vinavyoendeshwa na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas Italia, ujumbe wa shukrani kwa uwepo wao wa karibu pamoja na kuendelea kusali kwa ajili yake.

Watambue kwamba, kwa hakika anahitaji msaada wa sala zao katika kutekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Anawahakikishia kwamba, anawakumbuka katika sala zake na kuwatakia kheri na fanaka katika kipindi hiki cha Pasaka. Hayo yamebainishwa na Monsinyo Enrico Feroci, Mkurugenzi wa Caritas, Italia, alipokuwa anasoma ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa maskini wanaohudumiwa chakula na Caritas, Italia.

Watu hawa wanasema wameguswa kwa namna ya pekee na maneno ya Baba Mtakatifu Francisko anayesema kwamba, wao wanayo nafasi ya pekee kabisa katika moyo wake. Tarehe 27 Machi 2013, Caritas, Italia ilikuwa imemtumia Baba Mtakatifu Francisko ujumbe wa kheri na matashi mema pamoja na kumkaribisha miongoni mwao kama Askofu na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Watu hao wanaohudumiwa na Caritas wamejadiliana wao kwa wao kuhusu matukio kadhaa yaliyojiri ndani ya Kanisa: kung'atuka kutoka madarakani kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Conclave na hatimaye, kuchaguliwa kwa Papa Francisko.

Monsinyo Enrico Feroci ni kati ya Mapadre waliobahatika kupata chakula cha mchana pamoja na Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi kuu baada ya maadhimisho ya Ibada ya kubariki Mafuta Matakatifu.

Maskini wa Roma wanampongeza na kumshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kutokana na unyenyekevu ambao ameuonesha tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa, watu hawa wanasema, wataendelea kumsindikiza katika maisha na utume wake kwa njia ya sala. Wanamshukuru Mungu kwa kulipatia Kanisa zawadi ya Papa Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.