Waraka wa kichungaji wa Pacem in Terris, unatimiza miaka 50 tangu ulipoandikwa na
Papa Yohane wa XXIII
Ilikuwa ni tarehe 11 Aprili 1963 Papa Yohane wa ishirini na tatu alipochapisha Waraka
wa Kichungaji: "Pacem in Terris" yaani Amani Duniani, yapata miaka hamsini iliyopita.
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani, ameadhimisha tukio
hili kwa kutoa tafakari ya kina kuhusu: historia, umuhimu na changamoto zinazoendelea
kujitokeza ulimwenguni katika mchakato wa kulinda na kudumisha misingi ya haki na
amani katika kongamano la kimataifa lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Kikatoliki Marekani,
kuanzia tarehe 9 hadi 10 Aprili 2013.
Kardinali Turkson anabainisha kwamba,
Baba Mtakatifu Francisko ameamua kuchagua jina hili kwa kuzingatia mambo makuu manne:
vita, amani, umaskini na utunzaji bora wa mazingira. Haya pia ndiyo mawazo makuu yaliyojitokeza
yapata miaka hamsini wakati Baba Mtakatifu Yohane wa ishirini na tatu alipoandika
Waraka wake wa kichungaji, Amani Duniani, akiwa na picha ya kinzani, migogoro na vita
mara tu baada ya athari za vita kuu ya Pili ya dunia iliyoleta maafa makubwa na mwendelezo
wa vita baridi kati ya Mataifa makubwa duniani.
Aliona kwamba, amani ilikuwa
hatarini kutoweka na kwamba, kulikuwa kuna haja ya kujenga na kuimarisha misingi ya
umoja na udugu kwa kuaminiana, sanjari na utunzaji bora wa mazingira kama sehemu ya
mwendelezo wa kazi ya uumbaji.
Kardinali Turkson anasema kwamba, kiini cha
Waraka wa Kichungaji wa Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu ni: maisha, utu
na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Haya ni mambo ambayo
yanapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika sera na mikakati ya maendeleo endelevu
na kama sehemu ya kanuni msingi katika sheria na ushirikiano wa kimataifa. Huu ndio
msimamo ambao Vatican imekuwa ikiupatia msukumo wa pekee katika mikutano ya kimataifa
inayojadili masuala ya haki, amani na upigaji rufuku wa silaha za mahangamizi.
Baba
Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu wakati anaandika Waraka huu wa kichungaji ambao
unaendelea kuwa rejea katika kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na usalama
wa kimataifa, aliona jinsi ambavyo dunia ilikuwa imegawanyika na kutawaliwa na vita
baridi iliyokuwa inaendeshwa na mataifa makubwa yaani: Marekani na Urussi kwa wakati
huo. Kulikuwa na vitisho vya mashambulizi ya silaha za kinyuklia, jambo ambalo lilijenga
hofu na mashaka makubwa miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa.
Baba Mtakatifu
Yohane wa Ishirini na tatu akasimama kidete kuwaambia wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa
kujenga na kudumisha misingi ya haki na amani duniani. Wakuu hawa wakasikia ujumbe
wake, amani na utulivu vikarejea tena, ingawa vita baridi iliendelea kufuka moshi
chini kwa chini!
Ndiyo mchango kama huu uliotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo
wa pili wakati wa uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, kwa kukazia: ukweli,
utu na heshima ya binadamu, uhuru na mshikamano wa kimataifa. Vita baridi ikafifia
mataifa yakaanza kuaminiana na kujadiliana kwa pamoja mustakabali wa Jumuiya ya Kimataifa.
Kardinali
Peter Turkson anasema, si nyakati zote sauti ya kinabii inayotolewa na Mama Kanisa
imeweza kusikilizwa kwani, wakati mwingine wameipuuza na viongozi wakawasha moto wa
vita, kiasi cha kuleta maafa makubwa. Kunako mwaka 2011 wakati wa mgogoro na kinzani
za vita nchini Pwani ya Pembe, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alimtuma
kwenda nchini humo kupeleka ujumbe wa amani, lakini kwa bahati mbaya hakuruhusiwa
kuingia nchini humo, akabaki na ameshikilia Ujumbe wa Amani kutoka kwa Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, kwa muda wa juma zima bila mafanikio, baadaye akarudi nao!
Makubwa haya!
Malengo ya Maendeleo ya Millenia pamoja na mambo mengine yanapania
kufuta umaskini duniani. Kardinali Turkson anasema kuna baadhi ya viongozi wa Jumuiya
ya Kimataifa walikuwa na mawazo potofu kwa kudhani kwamba, wanaweza kuondokana na
umaskini kwa kuwafutilia mbali maskini kutoka katika uso wa dunia.
Ikumbukwe
kwamba, maskini wanahitaji kuwezeshwa katika elimu ili kuondokana na ujinga, wanatakiwa
kujengewa uwezo wa kiuchumi ili kupambana na hali mbaya ya maisha yao na hatimaye
kujiletea maendeleo endelevu, wanapaswa kusaidiwa katika maboresho ya huduma ya afya
kama njia ya kuimarisha nguvu kazi katika uzalishaji mali! Huu ndio mwelekeo sahihi
wa kupambana na umaskini wa hali na kipato miongoni mwa watu maskini.
Kardinali
Tukrson anafafanua kwamba, Waraka wa Kichungaji wa Amani Duniani unautajiri mkubwa
wa Maandiko Matakatifu kuhusu amani, kuwa ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amempatia
mwanadamu na kwamba, amani ni jina linalomwelekea Mungu mwenyewe. Amani ni neno linalowakilisha
ukamilifu na lengo la maisha ya mwanadamu, kama anavyobainisha Yesu Mwenyewe kwa njia
ya maisha na utume wake.
Ikumbukwe kwamba, amani ni tunda la haki na mapendo.
Amani ni sehemu ya mchakato wa kila siku ya maisha ya mwanadamu inayojikita katika
utafutaji wa utaratibu wa muafaka kadiri ya mapenzi ya Mungu na kwamba, amani inapatikana
ikiwa kila mtu atajitahidi kutekeleza wajibu wake, kwa kuzingatia: ukweli, upendo,
upatanisho na sheria. Kushindwa kwa mchakato wa amani ni vita!
Kardinali Turkson
anawataka waamini na watu wenye mapenzi mema kujitajirisha na Mafundisho Jamii ya
Kanisa kuhusiana na amani na kwamba, Waraka wa Amani Duniani ni dira na mwongozo makini
katika mchakato wa kujenga na kuimarisha amani duniani, hasa wakati huu wa ulimwengu
wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Hii ni changamoto ya
kudumisha ushirikiano wa kimataifa unaooongozwa na kanuni ya auni kwa ajili ya kutafuta
mafao ya wengi, kulinda na kutetea haki msingi, utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu. Watu wana haki na wajibu wa kujenga na kuimarisha amani
kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika haki msingi za binadamu na maendeleo endelevu
yanayozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.
Kama anavyosali Mtakatifu
Francisko wa Assisi, kila mtu anapaswa kuwa kweli ni chombo cha amani. Jumuiya ya
Kimataifa isimame kidete kuwalinda na kuwatetea maskini kwa kuwa kweli madaraja ya
amani na wala si kinzani, migogoro na vita vinavyosababisha maafa makubwa kwa Jamii.
Watu wajenge na kuimarisha utamaduni wa majadiliano unaosimikwa katika ukweli, heshima
na mafao ya wengi. Viongozi wa kidini wanapaswa kuonesha utashi wa kufanya majadiliano
ya kina, ili amani iweze kutawala na kudumu mioyoni mwa watu.
Kwa maneno haya,
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani alikuwa anahitimisha
tafakari yake kwa kukazia ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Pasaka alipokuwa
anatoa baraka na ujumbe kwa mji wa Roma na dunia kwa ujumla, kwa kukazia amani na
kuwataka watu wote wajitahidi kuwa ni vyombo vya huruma, upendo na msamaha wa Mungu.
Jumuiya ya Kimataifa bado inakabiliwa na roho ya ubinafsi, uchu wa mali na madaraka;
biashara haramu ya binadamu pamoja na uharibifu mkubwa wa mazingira.
Miaka
hamsini ya Waraka wa kichungaji, Pacem in Terris, Amani Duniani, iwe ni fursa kwa
waamini na watu wenye mapenzi mema, kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya
haki na amani duniani.
Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya radio Vatican.